SIMBA kweli imedhamiria kufanya makubwa katika msimu ujao wa Ligi Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya jana Ijumaa kushusha kiungo Mzambia, Chama Claytous anayekipiga Klabu ya Power Dynamos ya nchini humo.
Kutua kwa Mzambia huyo, kunafikisha wachezaji tisa wa kigeni waliokuwepo Simba kwa sasa. Wengine ni James Kotei, Asante Kwasi, Nicholas Gyan, Haruna Niyonzima, Meddie Kagere, Emmanuel Okwi, Pascal Wawa na Fabrice Mugheni.
Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 27 na uzito wa kilo 65, pia anachezea timu ya taifa ya Zambia ‘Chipolopolo’ na ana sifa kubwa ya kupiga krosi safi na pasi za mwisho hali itakayowafanya washambuliaji wa Simba, John Bocco na Meddie Kagere kuwa na nafasi ya kutupia tu mpira nyavuni.
Staili yake ya uchezaji inafananishwa na Okwi ambaye yupo ndani ya kikosi cha Simba kwani anaweza kumiliki mpira na kufunga mabao kwa mashuti ya mbali.
Kwa mujibu wa taarifa ambazo Championi Jumamosi imezipata ni kwamba, kiungo huyo alitua nchini jana Ijumaa akitokea nyumbani kwao Zambia kabla ya kupelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar kwa ajili ya kufanyiwa vipimo.
Mtoa taarifa huyo alisema, kiungo huyo alitarajiwa kusaini mkataba wa miaka miwili jana usiku baada ya kufanyiwa vipimo na kugundulika afya yake ipo vizuri.
Aliongeza kuwa, kiungo huyo aliyewahi kuicheza Zanaco ya Zambia, anatarajiwa kuwepo kwenye msafara wa Simba utakaoelekea Uturuki kwa ajili ya kambi ya wiki mbili.
“Leo (jana) amekuja kiungo mpya anayetarajiwa kusaini mkataba usiku baada ya kumalizika kwa mazungumzo kati yake na uongozi wa Simba kabla ya kusaini.
“Kiungo huyo ni kati ya wachezaji waliokuwepo Hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya kufanyiwa vipimo vya afya kabla ya kuanza safari ya kuelekea Uturuki tutakapokwenda kuweka kambi ya pamoja.
“Usajili wa kiungo huyo ni kati ya mapendekezo yaliyotolewa na benchi letu la ufundi katika kukiimarisha kikosi chetu katika kuelekea Ligi ya Mabingwa Afrika ambacho kinahitaji kuwa na wachezaji wenye uzoefu,” alisema mtoa taarifa huyo.
Kwa upande wake Kocha Mzambia aliyewahi kuinoa Yanga, George Lwandamina alisema kiungo huyo ni mzuri na ana sifa ya kufunga mabao makali ‘ya kideoni’ kwa umbali mkubwa muda wowote awapo uwanjani na pia ana ufundi wa kukaa na mpira pamoja na kupiga chenga.
Kaimu wa Rais wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’, juzi wakati akimtambulisha kocha mkuu wa kikosi hicho, Patrick Aussems raia wa Ubelgiji, alisema: “Kocha amekiona kikosi chake katika michuano ya Kagame na kuona baadhi ya upungufu ambao anahitaji kuuboresha na tayari mapendekezo hayo ameyakabidhi kwa uongozi na hivi sasa tunafanyia kazi.”
Sweetbert Lukonge na Wilbert Molandi
Comments are closed.