The House of Favourite Newspapers

Raia Adaiwa Kuuawa kwa Risasi na Polisi

MTU mmoja  ambaye jina lake halikufahamika mara moja, amefariki dunia baada ya kudaiwa kupigwa risasi na polisi eneo la Masika, Morogoro Mjini majira ya saa 4 usiku jana Novemba 6, 2018.

 

Kwa mujibu wa mashuhuda, inadaiwa palikuwa watu wawili ambao walionekana wamelewa pombe na walipofika eneo la Masika karibu na benki wakaanza kugombana, ndipo askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) aliyekuwa zamu lindoni katika benki hiyo akawafukuza.

 

Inadaiwa kwamba, kila mmoja alikimbia kivyake ambapo mmoja alielekea kwenye uchochoro wenye giza nene. Imedaiwa pia kwamba, askari huyo alifyatua risasi ambayo ilipenya kwenye banda la video na kumpata raia mmoja aliyekuwa amekaa kwenye benchi la mbele akitazama mechi ya mpira, ambapo ilimpiga kichwani na kufariki dunia papohapo.

 

Polisi walifika eneo la tukio muda mfupi baadaye na kufunga uzio ili watu wasiingie humo ambapo waliufanyia uchunguzi mwili huo.

 

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Wilbrod Mutafungwa, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema jeshi hilo linaendelea na uchunguzi zaidi na mwili umepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro.

UTASHANGAA: Muuza Mkaa Anavyomsomesha Rubani

Comments are closed.