The House of Favourite Newspapers

Rais Samia Afanya Mageuzi Makubwa Miradi ya Maendeleo Bukombe: Dkt Biteko

0

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ametajwa kuwa kiongozi mahiri katika kipindi cha muda mfupi huku akionyesha mageuzi makubwa ya Maendeleo.
Katika kipindi cha muda mfupi aliokaa madarakani kazi aliyoifanya haina mfano wake, hivyo watanzania wametakiwa kuendelea kumuamini na kumpa muda kwani kuna mambo makubwa ya maendeleo anaendelea kuyafanya.
Hayo yameelezwa na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa ambaye pia ni Waziri wa Madini Mhe Dkt Doto Mashaka Biteko wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika eneo la Runzewe katika wilaya ya Bukombe ikiwa ni muendelezo wa mikutano inayoandaliwa na CCM Mkoa wa Geita kueleleza utekelezaji wa ilani ya uchaguzi mwaka 2020-2025 katika majimbo yote ya mkoa huo.
Amesema kuwa katika kipindi kifupi, Ujenzi wa barabara, Miundombinu ya elimu, Afya, Maji, na huduma zote kwa wananchi zimeimarika hivyo Rais Samia anatakiwa kupimwa kwa kipimo cha mapenzi mema kwa watanzania, kwenye uendelezaji wa miradi ya maendeleo, kwa kuleta utulivu katika nchi, pamoja na kuimarisha Demokrasia nchini.
“Rais Samia amewafanya watanzania kila mmoja kujiona daraja la kwanza kwenye nyanja zote za Kilimo, Biashara, madini n.k mama huyu amepiga kazi kubwa sana” Amekaririwa Mhe Biteko
Dkt Biteko amesema kuwa tangu amechaguliwa kuwa mbunge ataendelea kuwa wakili mwaminifu kutoa ushuhuda kwa wananchi kwa mambo yaliyofanywa na Rais Samia katika Jimbo la bukombe.
Amesema Jimbo la Bukombe kabla ya CCM kushika hatamu liliwahi kuongozwa na upinzani na ilikuwa wilaya ya mwisho kwenye kila eneo kwenye sekta mbalimbali za maendeleo katika mkoa wa Geita.
“Kwa sasa wilaya inapaswa kupimwa kwa namba unaweza ukamchukia Rais Samia lakini namba zikamtetea, wilaya yetu tumetoka kwenye zahanati tatu sasa kuna zahanati 11, maboma mapya ya zahanati mpaka sasa ambapo maboma 22 yanajengwa, kutoka vituo vya afya viwili mpaka 7, kupandisha hadhi kituo cha Afya Uyovu kuwa hospitali”
“Tumerithi hospitali ya Wilaya ikiwa na hadhi kama zahanati tumeipandisha hadhi kwa kujenga majengo mapya, majengo ya dharula, jengo la mama na mtoto, tumetoka kuwa na shule moja ya kidato cha tano na sita mpaka kuwa nazo tano”
Kadhalika, Kuhusu utoaji wa leseni kwa upendeleo Mhe Biteko amesema kuwa hakuna upendeleo katika utoaji wa leseni kwa ajili ya uchimbaji wa madini nchini kwani leseni zote zinaombwa kwenye mfumo mtandaoni na hakuna kificho katika uombaji wa leseni.
Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini, Joseph Kasheku ‘Msukuma’ (kushoto) akiteta jambo na Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa  Mhe Dkt Doto Mashaka Biteko 
Leave A Reply