Rais Samia Ahutubia Taifa, Atangaza Kupungua kwa Bei ya Mafuta
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameongea na wananchi juu ya ongezeko la gharama ya bei ya mafuta na kugusia hatua ambazo Serikali imechukua ili kukabiliana na tatizo hilo.
Akiongea katika hotuba maalum akiwa Ikulujijini Dar es Salaam, Rais Samia amesema Serikali imechukua hatua ya kupunguza gharama za bei ya mafuta kwa kupunguza kodi kwenye sekta hiyo ili wananchi wapate unafuu ingawa amekiri kuwa kwa kufanya hivyo Serikali inapoteza mapato yake.
Rais Samia amesema kwa sasa watanzania wavumilie kwani mabadiliko hayo ya bei yataanza kutumika rasmi ifikapo June 01, 2022, amebainisha kuwa Waziri wa Nishati January Makamba pamoja na Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba watatoa taarifa Bungeni hivi karibuni kuhusu ni kwa namna gani Serikali imechukua hatua za madhubuti kukabiliana na tatizo hilo.
Akiongea moja kwa moja kutoka Ikulu, Rais Samia amesema wananchi lazima waelewe kuwa kupanda kwa gharama za maisha kumesababishwa kwa kiasi kikubwa na majanga mbalimbali yanayoendelea duniani ikiwemo vita kati ya Urusi na Ukraine.
Katika kufunga hotuba yake Rais Samia Suluhu Hassan amewapa pole wananchi juu ya adha hii na ongezeko la ugumu wa maisha na kusisitiza kuwa Serikali ipo makini kuhalkikisha inachukua kila hatua ili kupunguza ukali wa maisha kwa wananchi.