The House of Favourite Newspapers

RC Morogoro Afungua Mafunzo ya Tathmini Kwa Madaktari

0
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Martine Shigela, (aliyesimama) akitoa hotuba ya ufunguzi wa mafunzo ya siku tano kuwajengea uwezo Madaktari na Watoa Huduma ya Afya kutoka Mikoa ya Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Pwani na

MKUU wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Martine Shigela amewaasa madaktari wanaohudhuria mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kufanya tathmini za ulemavu uliotokana na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi kwa watumishi wa sekta ya Umma na Binafsi kufanya kazi hiyo kwa wepesi kwa weledi na kwa wakati ili wahusika waweze kupata fidia stahiki kama inavyopasa.

 

Mhe. Shigela ameyasema hayo leo Jumatatu Juni 14, 2021 mjini Morogoro wakati akifungua mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) na kuwaleta pamoja madaktari na watoa huduma za afya kutoka mikoa ya Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Pwani na Morogoro.

Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, akitoa hotuba ya utangulizi ili kuelezea historia ya Mfuko na lengo la mafunzo.

“Kufanya tathmini kunahitaji utaalamu, uelewa, ujuzi wa namna nzuri zaidi ya kufanya tathmini ili kuondoa malalamiko kwa anayefanyiwa tathmini, Tathmini ya mtu aliyelemaa si sawa na kufanya tathmini ya majengo, vyombo au mshine, tathmin ya binadamu ina changamoto na ndio maana WCF imeteua baadhi ya wataalamu ili kuja kupata mafunzo haya.” Alibainisha.

 

Alisema mafunzo hayo yataweza kujenga uwezo kwa wataalamu wengi hadi ngazi ya wilaya na hivyo kuwafikia watu wengi kwa wakati.

Aliusifu Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kwa kufanya kazi nzuri ambapo Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kupitia WCF imechangia kwa kiwango kikubwa kuwalipa watu wenye ulemavu uliotokana na ajali katika utumishi wao mahala pa kazi na hivyo umeweza kuzifanya familia ziweze kuendelea na maisha kama zilivyokuwa wakati mama au baba alivyokuwa na uwezo wa kawaida wa kuzalisha.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, WCF, Bi. Laura Kungenge akiratibu mafunzo hayo.

Lakini pia alitoa angalizo kwa waajiri kuhakikisha wanajisajili na Mfuko, kutoa taarifa sahihi za wafanyakazi na kutoa michango kwa wakati ili wafanyakazi waweze kunufaika endapo watapata matatizo wakat wakitekeleza majukumu yao ya kikazi.

 

Akimkaribisha Mkuu wa Mkoa kufungua mafunzo hayo, Mkurugenzi Mkuu wa WCF Dkt. John Mduma alisema mafunzo hayo ya siku tano ni kama sehemu ya hatua muhimu kuuwezesha Mfuko kutekeleza vema jukumu la kufanya tathmini sahihi na kwa wakati pindi mfanyakazi anapoumia au kuugua kutokana na kazi.

Sehemu ya washiriki wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi

“Mafunzo haya ni moja ya mikakati ya kuondoa changamoto ya kuwafikia walengwa kwa muda na kwa haraka na hivyo kutoa tathmini kwa wakati.” Alisema Dkt. Mduma.

Alisema wawezeshaji wa mafunzo hayo ni wataalamu wabobezi ambao wamekuwa wakishirikiana na Mfuko kuandaa miongozo ya tathmini ya ulemavu.

Aliwashukuru wataalamu (Wawezeshaji) na taasisi ambazo zimewaruhusu ili kushirikiana na Mfuko ambapo alizitaja kuwa ni pamoja na Hospitali ya Taifa Muhimbili, Hospitali ya Saratano ya Ocean Road, Hospitali ya Mifupa Muhimbili Chuo Kikuu Cha Sayansi Shirikishi MUHAS na Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi OSHA.

“Mfuko unatambua umuhimu wa mafunzo haya kwa watalamu na ndio maana yamepangwa kuwa endelevu na yamekuwa yakifanyika tangu Mfuko ulipoanza kutekeleza majukumu yake.” Alisema Dkt. Mduma.

Leave A Reply