The House of Favourite Newspapers

Sheva Ampa Ugumu Shiboub, Asogezwa Kwa Bocco

KOCHA Mkuu wa Simba Mbelgiji, Patrick Aussems ameonekana kunogewa na kiungo wake mshambuliaji mpya, Miraji Athumani ‘Sheva’ baada ya kumuhamishia namba 10.

 

Awali, nafasi hiyo ilikuwa inachezwa na nahodha wa timu hiyo John Bocco aliyekuwa nje ya uwanja kutokana na majeraha kabla ya baadaye kumtumia Msudan, Sharraf Eldin El Shivoub kwenye msimu huu.

Kiungo huyo aliyefunga mabao manne hadi hivi sasa wakati anatua kuichezea Simba katika michezo ya awali mitatu alikuwa akitokea benchi akicheza namba 7 na 11 kabla ya kuhamishiwa kwenye mchezo wa ligi na Biashara FC ya Mara.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Sheva alisema kuwa yeye nafasi halisi anayocheza ni namba 7 na 11, lakini ana uwezo kucheza namba 10 anayochezeshwa hivi sasa na kocha wake Aussems.

Sheva alisema kuwa kwanza anajisikia furaha kuaminiwa na kupewa nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza cha timu hiyo na kocha wake huyo baada ya michezo ya awali kuanzia benchi.

 

Aliongeza kuwa kucheza nafasi hiyo kumemfanya aongeze umakini na utulivu kila anapofika nje na ndani ya 18 kwa ajili ya kufunga, hivyo amewaahidi mashabiki wa timu hiyo kuendelea kufunga mabao katika ligi kuu.

“Kwa muda mrefu nilikuwa natamani kuanza katika kikosi cha kwanza na zilikuwa ndoto zangu za muda mrefu wakati ninajiunga na Simba katika msimu huu.

 

“Niliingia katika kikosi cha kwanza baada ya kocha na benchi la ufundi kwa jumla kuniamini na kocha Aussems kunipa mbinu za kufunga mabao ambazo hivi sasa zinaoenekana kuzaa matunda kwangu.

 

“Bado ninaendelea kurekebisha makosa yangu ambayo nimekuwa nikiyafanya na lengo langu ni kuendelea kufunga mabao bila ya kupanga idadi ili niipe ubingwa timu yangu ya Simba,” alisema Sheva.

Stori Na Wilbert Molandi Dar es Salaam

Comments are closed.