The House of Favourite Newspapers

Shule Ya St. Mary Goreti Yaotesha Miti 2000 Kilimanjaro

0
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mh. Kisare Makori (wa pili kulia) akipokea mche wa mfano kati ya miche 2000 kutoka kwa Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya St. Mary Goreti Sr. Clementina Kachweka ( kushoto) wakati wa uzinduzi rasmi wa kampeni ya upandaji miti ya shule hiyo. Wengine kutoka kushoto ni kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Dkt. Jar Khanga na Katibu Tawala wa Wilaya ya Moshi, Angela Marko.

Shule ya sekondari St. Mary Goreti iliyoko Moshi, mkoani Kilimanjaro, imepanga kuotesha miti 2,000 mkoani humo ili kuunga mkono juhudi za Serikali za kupanda miti na kurudisha uoto wa asili.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa shule hiyo Sr Clementina Kachweka wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kupanda miti ikiwa ni uzinduzi wa mpango huo, iliyofanyika katika viwanja vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Jumatatu.

“Mpango huu wa kupanda miti utakuwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa shule yetu yanayotarajiwa kufanya mwakani”, alisema na kuongeza shule hiyo inashirikiana na Benki ya NMB ambayo imechangia miche 1000 kati ya 2000.

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mh. Kisare Makori (katikati) akiotesha mti wa mfano huku akisaidiana na Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mary Goreti, Sr. Clementina Kachweka baada ya shule hio kukabidhi miche 2000 kwa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kama sehemu ya kampeni ya shule hiyo ya upandaji miti.

Alisema ili kutimiza azma hiyo, shule hiyo inatarajia kugawa miti katika wilaya zote za Mkoa wa Kilimanjaro ambayo itapandwa maeneo mbalimbali ya wilaya hizo kwa utaratibu utakaowekwa na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro.

“Kama tunavyojua, Makamu wa Rais Dr Philip Mpango alitangaza kuwa upandaji miti uwe ni kipaumbele cha kwanza hapa nchini, hivyo katika kuunga mkono juhudi za Serikali, tumeingiza mpango wa kupanda miti kama sehemu ya maadhimisho yetu ya miaka 25 ya shule yetu”, alisema.

Alitoa rai kwa wananchi wote kuunga mkono juhudi za Serikali za kupanda miti kutokana na ukweli kuwa miti ni sehemu ya maisha ya Binadamu.

“Miti ni muhimu katika utunzaji wa vyanzo vya maji ambayo binadamu wote tunayatumia kwa njia moja au nyingine kile siku, inatupatia vivuli na pia inatumika katika ujenzi wa nyumba tunazotumia kama makazi yetu kwa kutaja faida chache tu za miti”, alisema.

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mh. Kisare Makori (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa mkoa wa Kilimanjaro na uongozi na wanafunzi wa Shule ya St. Mary Goreti baada ya shule hio kukabidhi miche 2000 kwa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kama sehemu ya kampeni ya shule hiyo ya upandaji miti.

Akiongea katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Moshi Mh. Kisare Makori aliupongeza uongozi wa shule hiyo kwa kuja na mpango wa kupanda miti na hivyo kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha mazingira na kurudisha uoto wa asili.

“Upandaji wa miti 4,000 ndani ya Mkoa wa Kilimanjaro ni hatua kubwa katika kuboresha mazingira na pia katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ambayo yamekuwa ni changamoto kubwa katika miaka ua hivi karibuni”, alisema.

Mh. Makori, ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw Nurdin Babu katika hafla hiyo, alisema kuwa maboresho ya mazingira ni muhimu kutokana na ukweli ndiyo chanzo cha ubora ya maisha ya wanadamu kwa njia moja au nyingine.

“Tusipoboresha mazingira yetu wakati idadi ya watu inazidi kuongezeka hali haitakuwa nzuri kutokana na ukweli watu wanategemea maisha yao kuwa mazuri pale mazingira yanapokuwa mazuri kutokana na ukweli mazingira mazuri yanayotokana na uweko wa miti ni chanzo cha hali ya hewa nzuri na rafiki kwa wanadamu”, alisema.

Alitoa rai kwa taasisi zingine za kielimu, taasisi binafsi, zile za umma na wadau wengine wa maendeleo kuiga mfano wa shule ya St Maria Goreti kwa kuanzisha kampeni za upanda miti na utunzaji wa mazingira kwa ujumla ili kuboresha mazingira kwa kurudishia uoto wa asili.

Wakati wa hafla hiyo, Bw Makori na Mkuu wa shule hiyo Sr Clementina walipanda mti mmoja kila mmoja ikiwa ni ishara ya uzinduzi huo ambao pia ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali nagazi ya mkoa na wilaya, viongozi wa shule ya St. Mary Goreti, walimu, wafanyakazi na wanafunzi.

Shughuli zote za St. Mary Goreti kuelekea sherehe za miaka 25 zinaratibiwa na kampuni ya Executive Solutions Limited, moja ya makampuni yanayoongoza katika kuandaa matukio mbalimbali na uratibu wa masuala ya habari.

Leave A Reply