The House of Favourite Newspapers

Simba wamshtukia Majabvi, wamkata mshahara

0

majadviKiungo wake mkabaji Mzimbabwe, Justice Majabvi.

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

KUTISHIA kumtimua haikutosha, uongozi wa Simba umeamua kumkata mshahara wa mwezi huu kiungo wake mkabaji Mzimbabwe, Justice Majabvi.

Hiyo ni siku chache tangu kiungo huyo alipoujia juu uongozi wa timu hiyo akilalamikia kutotimiziwa mahitaji yake kwa mujibu wa mkataba tangu ajiunge na Simba, hasa suala la malazi.

Uongozi wa Simba ulikasirishwa na kitendo hicho na kuchukua uamuzi wa kumtimua nyota huyo mwenye mkataba wa miaka miwili ambaye ni tegemeo kwenye kikosi hicho kinachonolewa na kocha Dylan Kerr.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara, alisema uamuzi huo wa kumkata mshahara umekuja kutokana na Majabvi kuvunja makubaliano ya mkataba ya kuzungumza na vyombo vya habari bila ruhusa ya uongozi.

Manara alienda mbali zaidi kwa kusema: “Tumeshtuka kuwa anachokifanya Majabvi ni mchezo mchafu unaochezwa na moja ya klabu kubwa hapa nchini ambayo ina matatizo na kiungo wao.”

Yanga ndiyo yenye matatizo na kiungo wake Haruna Niyonzima raia wa Rwanda ambaye amesimamishwa kwa kosa la kuchelewa kuripoti katika timu yake kutoka Rwanda alipokuwa akiitumikia timu ya taifa.

“Kila kitu kina utaratibu wake, Majabvi amekiuka makubaliano yaliyokuwepo kwenye mkataba ambao haumruhusu kuizungumzia klabu kwenye vyombo vya habari.

“Kutokana na kosa hilo, kama uongozi tumechukua uamuzi wa kumkata nusu ya mshahara wake atakaoupokea mwezi huu. Kuna timu inamtaka Majabvi kuziba pengo la mchezaji wao, hivyo tumewashtukia,” alisema Manara.

Leave A Reply