Simba Yamtambulisha Kocha Mpya Zoran Maki, Adai Yupo Tayari kwa Dabi Dhidi ya Yanga
KLABU ya Simba imemtambulisha Kocha wao mpya Zoran Maki mbele ya waandishi wa habari na kuanika mipango yao mipya kuelekea msimu mpya wa ligi wa 2022/2023.
Kocha Zoran amesema amefanikiwa kufanya vizuri katika Ligi mbalimbali alizofanya kazi ambapo amesema amefanikiwa kutinga katika nusu fainali mbili za Ligi ya Mabingwa Barani Afrika huku pia akifanikiwa kutinga katika robo fainali nne za mashindano hayo.
Kuhusu upinzani uliopo kati ya Simba na Yanga Zoran amesema kila nchi aliyofanya kazi amekutana na dabi mbalimbali hivyo Simba na Yanga hazina tofauti.
“Kila nchi niliyofanya kazi kumekuwa na hizi Dabi Morocco kuna Wydad na Raja Casablanca zaidi ya mashabiki elfu 70, Sudan Hilal na El Mereikh elfu 50 Algeria elfu 40 kwahiyo lazima tufanye maandalizi kwa dabi, hata hapa pia natambua kuna Dabi kubwa Simba na Yanga tunao muda na tutajiandaa kwa ajili ya mchezo huo.”
Simba na Yanga zinatarajiwa kuumana katika mchezo wa ngao ya jamii unaotarajiwa kuchezwa Agosti 13 mwaka huu katika Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
Wakati huohuo Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Klabu ya Simba Ahmed Ally amesema klabu hiyo inatarajiwa kuondoka nchini Julai 14, 2022 kuelekea nchini Misri kwa ajili ya kuweka kambi ya takribani wiki nne ya maandalizi ya msimu mpya wa 2022/2023 kabla ya kurejea nchini Agosti 5, 2022 kwa ajili ya maandalizi ya Simba Day.