The House of Favourite Newspapers

Siri Bata la Zari Dubai Yaanikwa

Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’

DAR ES SALAAM: Wakati suala la mzazi mwenzake Nasibu Abdul ‘Diamond’, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ kutanua pande za Dubai likidaiwa kuwezeshwa na kigogo mmoja, imebainika tofauti na maneno ya watu mitandaoni.

Kwa takriban wiki moja na zaidi, Zari ameonekana Dubai akiwa na wanaye wakubwa watatu, wakila bata katika viunga mbalimbali vya kuponda raha hali iliyofanya watu wengi kutoa maoni yao mitandaoni.

Kuna baadhi ya watu walimsifia kwa kueleza kuwa anachokifanya ni sahihi kwani anao uwezo wa kifedha hivyo kula bata si tatizo, tofauti na wanawake wenzake waliowahi kutoka na Diamond, Wema Sepetu na Hamisa Mobeto.

Kuna wengine walimponda kwa madai kuwa fedha hizo anazotumia, si zake bali kuna kigogo anayemwezesha hivyo asijishebedue na kuwarusha roho kina Wema na Mobeto.

Risasi Jumamosi lilifanikiwa kuzungumza na mtu wa karibu na Zari ambaye aliomba hifadhi ya jina na kubainisha, licha ya Zari kuwa na fedha zake lakini nyuma ya safari yake hiyo, yupo mdhamini anayemwezesha.Alisema, safari hiyo Zari amedhaminiwa na kampuni moja (jina kapuni) ambaye ndiye anayempa jeuri hiyo.

“Watu hawajui tu. Nimeona wanasema mengi sana mitandaoni, ooh sijui kuna kigogo sijui Zari hana pesa ya kukaa Hoteli ya Dusit Marina pale Dubai, kwanza watambue Zari ana fedha.

“Mtu anamiliki mashule, ana maduka Afrika Kusini atashindwa kulipia hoteli shilingi milioni tano kwa siku? (Chumba cha hoteli hiyo gharama yake kwa siku ni kati ya shilingi laki 5 na milioni moja na ushee),” alisema mtu huyo wa karibu na Zari.

Kama hiyo haitoshi, mtu huyo aliweka bayana kuwa licha ya kujimudu kifedha, safari hiyo Zari alidhaminiwa na ndio maana hata picha alizoposti kwenye mtandao wa Instagram, amewataja wadhamini.

Risasi Jumamosi liliingia kwenye kurasa mbalimbali katika mtandao wa Instagram na kukutana na kampuni hiyo iliyomdhamini Zari.

Hadi tunakwenda mitamboni juzi, imeelezwa kuwa Zari pamoja na wanaye watatu wakubwa pamoja na kijana mwingine, walikuwa bado wapo Dubai wakitumbua maisha.

STORI: MWANDISHI WETU, RISASI JUMAMOSI

Comments are closed.