The House of Favourite Newspapers

STAMINA AMSIKITISHA TUNDA BAADA YA KUOA

Stamina

POPOTE watakapozungumziwa wanamuziki wakali wenye mchango mkubwa kwenye gemu la Muziki wa Bongo Fleva, bila shaka jina la Tunda Man, haliwezi kuachwa kutajwa.

Si rahisi kuachwa kutajwa kwa sababu mwanamuziki huyu kutoka mitaa ya Manzese, Tip Top Connection, hakika ana mchango mkubwa kwenye gemu kwani amefanya kazi nyingi na wanamuziki wakubwa zilizoweza kumpa jina na heshima.

Amefanya kazi na Chid Benz, Matonya, Chege, Temba, Ali Kiba, Madee, Spack na wanamuziki wengine wengi ambao waliwahi kufanya vizuri au bado wanaendelea kufanya vizuri kwenye tasnia ya muziki Bongo.

Hata hivyo baada ya kufanya vizuri, takribani miaka mitatu Tunda yupo nje ya gemu. Alikuwa amepotea, akibakia kuahidi ahadi nyingi ambazo alikuwa hatekelezi. Zikiwemo; ‘nitarudi soon’ lakini miaka ndiyo hivyo ikawa inakatika.

Lakini hivi karibuni Tunda amerudi kwenye gemu. Tena kwa hasira kwelikweli maana ameibuka na ngoma tatu ambazo ni Bosi Hanuniwi, Kwigoda na Mama. Kutokana na kishindo hicho, Mikito Nusunusu, iliamua kumtafuta ili kuweza kupiga naye stori juu ya kurudi kwake, kilichompoteza kimuziki na mambo mengine mengi. Huyu hapa kwenye mahojiano;

Mikito: Mzee umerudi kwa kishindo kwelikweli.

Tunda: Ni kweli, unajua nilikaa kimya muda mrefu, sasa nimeona nirudi kwa namna hii ili kuweza kukata kiu ya mashabiki wangu.

Mikito: Lakini kibiashara hii imekaaje, huoni huzipi nafasi nyimbo kuachiana muda wa kuzoeleka kwa mashabiki?

Tunda: Hapana. Kila wimbo una utofauti wake. Ukitazama hata kwenye Mtandao wa YouTube, nyimbo zote zimepokelewa vizuri na zimetazamwa na watu wengi. Kwa hiyo kuna uwezekano kabisa mashabiki wakawa wanasikiliza nyimbo zote na wala haina shida.

Mikito: Umetoa nyimbo tatu kwa sababu ndiyo unarudi au huu ndiyo utakuwa utaratibu wako mpya?

Tunda: Huu ndiyo utaratibu wangu mpya. Kwa sasa kila nikiachia ujio mpya nitakuwa naachia video tatu. Na utaratibu huu utaitwa ‘T-hatrick’, yani Tunda hatrick

Mikito: Unafikiri ‘impact’ ya staili yako hii mpya itakuwa nini?

Tunda: Kwanza nitarudisha kupata shoo nyingi kuliko ilivyokuwa hapa katikati. Lakini pia nitazungumziwa zaidi na mashabiki, watakuwa wanasikiliza nyimbo zangu mimi zaidi na ukizingatia hakuna mwanamuziki amewahi kufanya jambo hili. Kwa hiyo mimi naona impact yake ni kubwa tu!

Mikito: Tukirudi kwenye kupotea kwako, nini hasa kilicho kupoteza?

Tunda: Kiukweli ni masuala ya kifamilia. Unajua nimeoa takribani mwaka mmoja na nusu uliopita. Sasa baada ya kuoa ilikuwa ni lazima niipate heshima ya ndoa ambayo ni mtoto. Ninamshukuru Mungu nimebahatika kupata mtoto wa kike takribani wiki kama tatu zilizopita, anaitwa Insar.

Mikito: Kwa hiyo unataka kutuambia kwamba kuoa inaweza kuwa chanzo cha mwanamuziki kupotea?

Tunda: Hapana. Siyo hivyo. Ingawa inategemeana na mwanamke uliyemuoa ni wa namna gani. Ila kweli kuna muda unafika baada ya kuoa unakaa kimya ili kuipata heshima ya ndoa, mke akuzoee na kutengeneza ukaribu zaidi. Kwa mfano juzikati ndugu yangu Stamina amenisikitisha sana, baada ya kuoa tu amekwenda kupiga shoo. Si kitu kizuri unapooa ni lazima umpe yule mwanamke muda wa kukaa naye maana shoo zipo tu unaweza kuzifanya wakati wowote na muda wowote.

Mikito: Lakini muziki ni kama ajira, mtu kukaa nje kwenye ajira yake kwa takribani mwaka kutengeneza tu heshima ya ndoa huoni ni muda mrefu?

Tunda: Ni kweli, lakini bado kuna namna ambavyo muziki unaweza kuendelea kukuingizia kipato ukiwa karibu na familia yako. Ni wewe tu mwenyewe namna ambavyo utaamua kufanya maisha yako.

Mikito: Kwa kumalizia mipango yako mingine ya kimuziki kwa sasa ipo vipi?

Tunda: Ni mikubwa, ndiyo kama nilivyosema kwamba nimerudi tena kwa kishindo, kwa hiyo mashabiki wangu wategemee makubwa zaidi maana ni mwendo wa ‘T-hatrick.’

Makala: Boniphace Ngumije

Comments are closed.