The House of Favourite Newspapers

Stars kuwakanyaga Wasudani kesho

KAIMU Kocha Mkuu wa  Taifa Stars, Mrundi, Etienne Ndayiragije amesema kuwa wamejipanga vizuri kuhakikisha wanaibuka na ushindi katika mchezo wa kuwania kufuzu fainali za wachezaji wa ndani Chan dhidi ya Sudan.
Stars kwa sasa inakibarua kigumu kwa wachezaji wanaocheza ligi ya ndani kufuzu fainali za Chan zinazohusisha wachezaji wa ndani inayotarajia kufanyika nchini Cameroon mwaka 2020.

 

Stars itacheza na Sudan kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar baada ya kufanikiwa kuwatoa Kenya katika mchezo wake wa kwanza wa hatua ya mtoano. Akizungumza na Championi Jumamosi, Ndayiragije alisema
kuwa wamejipanga vizuri kwa kuhakikisha wanapata matokeo katika mchezo huo kutokana na kufahamu mbinu za wapinzani wake.

“Tunaendelea na maandalizi vizuri kwa sababu kikubwa ninachokiangalia wachezaji wangu wameingiza kitu katika mazoezi, hakuna mtu asiyefahamu juu ya muda kuwa mdogo lakini tunapambana kwa kuhakikisha tunawafunga wapinzani wetu.

 

“Unajua hizi mechi zinachezwa kwa mtindo wa mtoano sasa kama mwalimu naangalia ni jinsi gani nawapa kitu vijana wangu ili waweze kushinda kitu ambacho kwetu kinawezekana kutokana na maandalizi yetu,” alisema Ndayiragije. Kwa upande wa Kocha Mkuu wa Sudan, Zdravko Logarusic raia wa Crotia alisema kuwa  amekuja nchini kwa kazi moja ya kuhakikisha anaifunga Stars katika mchezo huo kutokana na  maandalizi makubwa waliyofanya.

 

“Tupo hapa kwa kazi moja kuhakikisha tunashinda si chini ya mabao matatu, tumejipanga vyema na sina wasiwasi kabisa na kikosi changu kwa kuwa tayari tumeshafuz fainali za Kombe la Dunia,” alisema Logarusic ambaye amewahi kuinoa Simba.

Comments are closed.