Taasisi ya Wananchi Wazalendo Tanzania (TWWT) Yatoa Elimu ya Kizalendo UDART
TAASISI ya Wananchi Wazalendo Tanzania (TWWT) ikiongozwa na Mwenyekiti wake Dkt. Ezekiel Kyogo na Makamu wake, Dkt. Nuru Kalufya inayoendelea kutoa elimu ya uzalendo sehemu mbalimbali wiki hii imetoa kwa wafanyakazi wa mradi wa mabasi yaendayo kasi jijini Dar UDART.
Katika mafunzo hayo, Dkt Ezekiel aliambatana wakufunzi wenzake Dkt. Riziki na Dkt. Nuru ambao ni wahadhiri wa Chuo cha Ustawi wa Jamii ambao wote kwa pamoja walitoa elimu ya kizalendo kwa wafanyakazi hao.
Katika msafara huo wa TWWT pia alikuwepo Mkuu wa Dawati la Jinsia Kituo cha Polisi cha Msimbazi, afande Eva Simon ambaye naye alitoa elimu ya uzalendo na kuelezea jinsi watu wa jinsi tofauti mnavyotakiwa kuishi kizalendo pasipo kukwazana.
Akitoa elimu kwa wafanyakazi hao, Dkt. Ezekiel aliwaeleza umuhimu wa uzalendo kwa taasisi wanayofanyia kazi kwa ajili ya maendeleo ya taasisi hiyo na taifa kwa ujumla. Dkt. Kyogo alisema;
“Unakuta derava wa basi la mwendokasi kwakuwa unajua uko barabara yako basi ukiona chochote mbele yako awe dereva wa bodaboda, gari jingine basi wewe unampelekea tu ukijiamini kuwa utaonekana huna kosa upande wako.
“Sawa unaweza kweli usiwe na kosa lakini kumbuka ni lazima katika ajali hiyo utakuwa umeharibu barabara au basi unaloendesha na kumsababishia madhara uliyemgonga na pengine vifo hata kama aliyemgonga ndiye mwenye makosa, tuwe wazalendo jamani” alisema Dkt. Ezekiel.
Baada ya kutoa elimu ya kutosha kwa wafanyakazi hao aliingia Dkt. Riziki ambaye naye alianza kutoa elimu hiyo. Pamoja na mambo mengine, Dkt. Riziki aliwaeleza wafanyakazi hao umuhimu wa kufanya kazi kizalendo na kuacha alama ya ushindi.
Aliwaambia kuwa unapofanya kazi kwenye taasisi na ikafa hata thamani yako unapotaka kwenda kuomba kazi sehemu nyingine si rahisi kupewa heshima. Dkt Riziki alisema;
“Hivi mfano ulifanyakazi kwenye shirika fulani halafu likafa hivi unajisikiaje unapoenda kuomba kazi sehemu nyingine? “Je, Unaweza kujitambulisha kuwa mimi ndiye nilikuwa mfanyakazi wa ile taasisi iliyokufa? “Si utaambiwa ahaaa… nyie kumbe ndiyo wale mliyeliua lile shirika!! “Nafikiri itakuwa ni aibu kwenu hivyo fanyeni kazi kizalendo ili muache alama ya ushindi wa kujivunia popote muendapo”. Alimaliza kusema Dkt. Riziki.
Baada ya elimu hiyo kutoka kwa Dkt. Riziki aliingia Dkt. Nuru ambaye alitoa elimu ya kuishi kizalendo kama ifuatavyo;
“Mengi yamezungumza na wakufunzi waliotangulia lakini mimi napenda kuwaeleza umuhimu kuheshimiana katika kuishi kizalendo. “Unakuta mwingine unakosa uzalendo na kuanza kudhalilisha wenzako wa jinsia tofauti na kuwafanya washindwe kufanya kazi kizalendo”. Alisema Dkt Riziki.
Baada ya kusema hayo, Dkt Riziki alitaka kujua kama ndani ya shirika la UDART kuna dawati la jinsia na alijibiwa kuwa lipo hivyo aliwataka wanaopatwa na changamoto ya kukumbana na unyanyasaji huo wasikose kulitumia dawati hilo.
Katika mafunzo hayo mwingine aliyepata nafasi ya kuzungumza ni Mkuu wa Dawati la Jinsi Kituo cha Polisi Msimbazi, Eva Saimon ambaye aliwahasa wafanyakazi hao kuishi kizalendo na kuepuka kunyanyasana kijinsia.
Baada ya elimu hiyo wafanyakazi wa UDART nao walipata nafasi ya kuuliza maswali na kuelezea changamoto wanazokumbana ambapo ziliahidiwa kutatuliwa.
HABARI/PICHA : RICHARD BUKOS NA ISSA MNALLY /GPL