The House of Favourite Newspapers

Tambwe Ataka Miezi Sita Yanga

ALIYEKUWA mshambuliaji wa Yanga, Mrundi, Amissi Tambwe ameutaka uongozi wa klabu hiyo kumpa mkataba wa miezi sita ili arudi kikosini kwa ajili ya kuondoa ukame wa mabao uliopo hivi sasa.

 

Tambwe ni mchezaji huru na yupo nyumbani kwao Burundi baada ya kuvunja mkataba na timu ya Fanja ya nchini Oman ambayo alijiunga nayo mwanzoni mwa msimu huu kutokana na kukabiliwa na matatizo ya kifamilia.

 

Tambwe alisema kuwa kutokana na ufiti alionao hivi sasa endapo Yanga watampatia hata miezi sita tu, anaamini atafanya mambo makubwa.

 

Alisema licha ya ufiti alionao lakini pia uwepo wa wachezaji wanaojua kupiga krosi kwa sasa katika kikosi hicho kama vile Juma Abdul, Patrick Sibomana na Mapinduzi Balama, anaamini kuwa atafunga mabao mengi kama ilivyokuwa msimu wa 2014/15 na 2015/16 alipokuwa akicheza na Simon Msuva, Haruna Niyonzina na Juma Abdul ambao ndio walikuwa wapishi wakuu wa mabao yake.

 

“Yanga kama wananihitaji nipo tayari kurudi kikosini hapo niwafanyie kazi kama ilivyokuwa wakati ule natoka Simba. “Uwezo wa kufanya hivyo ninao lakini pia uwepo wa Juma Abdul, Sibomana na Balama naamini nitafunga sana kwani ni wazuri kwa mipira ya krosi ambayo sasa hakuna mtu mahiri wa kuitumia,” alisema Tambwe.

 

Rekodi zinaonyesha katika msimu mitano aliyoitumikia Yanga, Tambwe alifunga mabao 52 ambapo mabao 35 aliyafunga msimu wa 2014/15 na 2015/16 wakati alipokuwa fiti kabla ya kusumbuliwa na majeraha ambayo yalimweka nje ya uwanja kwa muda mefu lakini hivi sasa amepona na yupo fiti

Sweetbert lukonge, dar es Salaam

Comments are closed.