The House of Favourite Newspapers

Ulevi huu ni mbaya kuliko ule wa Kitwanga

0

kitwangaAliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga.

LIMETOKEA jambo baya katika nchi yetu linaloweka historia kwa kiongozi wa serikali, ngazi ya uwaziri kupoteza kazi kwa sababu ya ulevi. Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga amefukuzwa kazi na Rais Dk. John Magufuli kwa sababu ya mteule wake huyo kuzidisha kilevi kilichomfanya kushindwa kutimiza majukumu yake sawasawa.

Kuna mambo mengi yanazungumzwa juu ya hatua iliyochukuliwa, wengi wakimpongeza rais kwa nia yake ya dhati ya kuhakikisha watumishi wa umma wanafanya kazi kwa maadili, uwajibikaji na nidhamu.

Ni kweli kwamba kuna kundi kubwa la watu wanaokunywa pombe, baadhi yao wakipitiliza na kujikuta wakishindwa kufanya kazi au kufanya vyema katika majukumu yaliyo mbele yao, lakini pia wakishindwa kuweka sawa mambo yao.

Lakini ulevi wa pombe una madhara kidogo sana kwa jamii yetu kuliko ulevi wa madaraka walionao viongozi wengi katika serikali yetu. Hapa ninazungumzia watu kama wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa idara, wakuu wa mikoa, maofisa wakubwa mikoani, wakurugenzi walio wizarani, manaibu mawaziri na hata mawaziri wengine.

Ulevi huu wa madaraka upo pia hadi kwa maofisa watendaji wa ngazi za vijiji na kata, achilia mbali watu waliopewa dhamana ya kulinda uhai wa watu kama madaktari na polisi.

Kabla ya kuingia madarakani kwa serikali hii ya Magufuli, wananchi walikuwa wakiteswa sana na kauli kama ‘unajua mimi ni nani?’.

Kauli hizi zilitolewa na viongozi hao wakati wananchi wakiwa wanahitaji huduma zao, lakini wanacheleweshewa au kunyimwa. Mbaya zaidi, wakati mwingine zinatolewa hata na watoto wao, vimada wao, wake zao, wajomba zao au wategemezi wengine kwa sababu tu waziri, mkuu wa mkoa au bosi wa mamlaka ni baba, mjomba, shangazi au unasaba mwingine.

Ulevi huu upo sana kwa viongozi wa serikali, wanataka wananchi wawaogope, wakienda kutaka huduma, wanyenyekewe, wakati ukweli ni kwamba wanaopaswa kunyenyekewa ni wananchi kwa sababu ndiyo waajiri.

Ni vyema, Rais Magufuli akamulika eneo hili na wananchi wapo tayari kumsaidia. Kuna mabosi wanafika kazini muda wanaotaka, wanafanya kazi pale wanapojisikia na wanatoa lugha za kejeli na masimango bila kujali kana kwamba ni shughuli zao binafsi.

Tunajua jeshi la polisi kwa mfano, linaendeshwa kwa fedha za walipa kodi, lakini siyo jambo la ajabu kwamba wananchi wanapokwenda kupeleka matatizo yao, baadhi ya askari waliolewa madaraka wanawalazimisha kutoa hela ya mafuta ili waende kufuatilia tatizo lake.

Shida kama hizi wanazipata karibu katika ofisi zote za umma ambazo zimewekwa kwa ajili ya kuwahudumia.

Ni afadhali ya ulevi wa pombe kwa sababu wanakunywa kwa pesa zao, lakini ulevi huu unawaumiza watu wasiostahili, tena katika ofisi za umma.

Vyema Rais Magufuli akautazama ulevi huu. Wananchi wanawajua watumishi wa umma waliolewa kilevi hiki na wako tayari kuwataja ili nao wawajibishwe kama ilivyotokea kwa Charles Kitwanga.

Nachochea tu!

KUNUNUA NA KUSOMA MAGAZETI YA GLOBAL PUBLISHERS ONLINE, INGIA HAPA==>VODACOM M-PAPER APP

*********

JIUNGE NA SOCIAL MEDIA ZETU

KWA HABARI ZA KITAIFA, KIMATAIFA, MASTAA NA MIKASA YA KUSISIMUA

INSTAGRAM: @Globalpublishers

ERIC SHIGONGO INSTAGRAM: @ericshigongo

TWITTER: @GlobalHabari

FACEBOOK: @GlobalPublishers

SUBSCRIBE YOU TUBE: Global TV Online

GLOBAL TV ONLINE: www.globaltvtz.com

HADITHI ZA KUSISIMUA NA MBINU ZA UJASIRIAMALI, ERIC SHIGONGO FACEBOOK PAGE:@shigongotz

Leave A Reply