VALENTINE’S DAY IMEPITA, UMEJIFUNZA NINI?
JANA ilikuwa ni Siku ya Wapendanao, au Valentine’s Day, siku ya kuonyesha upendo kwa yule umpendaye.
Bila shaka kila mmoja aliisherehekea kwa kadiri ya utashi wake.
Nilichokigundua, ambacho huwa pia nakishuhudia miaka yote, watu wengi hukaa kuisubiria siku hiyo eti ndiyo wawaonyeshe wapenzi wao kwamba wanawapenda na kuwajali, siku ikipita kila kitu kinakuwa kimeisha, hawajui kwamba mapenzi siyo kitu cha siku moja.
Kama kweli unampenda, siyo lazima usubirie Valentine’s Day ndiyo umuonyeshe kwamba unampenda, bali unatakiwa kumpenda na kumuonesha kwa vitendo kwamba unampenda kila siku!
Ukiwa ni mtu wa matukio, maana yake siku zote utakuwa unaishi na mwenzi wako kimazoea, unasubiri mpaka Valentine’s Day eti ndiyo unajifanya kuonyesha upendo wako. Kwa bahati mbaya, Valentine’s Day yenyewe inapita kama upepo, unaisubiri kwa siku nyingi, inakuja na kupita, unakaa na kuanza kusubiri tena ya mwaka mwingine.
Kama na wewe ni mtu wa aina hii, nakuhakikishia huwezi kudumu kwenye mapenzi, kila siku utakuwa ni mtu wa kulizwa tu na mapenzi. Kila siku inapaswa kuwa Valentine’s Day kwako, muonyeshe upendo, muonyeshe kumjali na mfanyie mambo mazuri kila mara.
Watu wengi huhisi kwamba ili wawe na maisha ya furaha na watu wanaowapenda, ni lazima wawe na fedha nyingi, wawanunulie vitu vya thamani, wawatoe ‘out’ kwenda viwanja vikubwau wawafanyie mambo makubwa. Kasumba hii wanayo zaidi wanaume ingawa wanawake nao siku hizi wameanza kuamini hivyo.
Hata hivyo, hiyo siyo tafsiri ya mapenzi ya kweli na kama utaacha kufanya mambo ya msingi ukaelekeza nguvu zako kumpa mwenzi wako fedha na vitu vya thamani, utakuwa sawa na mtu anayejenga nyumba ya kifahari juu ya mchanga.
Mapenzi yanajengwa kuanzia chini, ukishakuwa na msingi mzuri basi hayawezi kukusumbua lakini kama ukishindwa kusimamisha msingi imara, hata utumie kila kitu chako, bado hutaweza kumfurahisha mwenzi wako.
Mapenzi ni hisia, na mara zote hisia huanzia ndani ya moyo. Ni rahisi sana hisia za mapenzi kufa na inapotokea hivyo, hata kama mtu alikuwa anakupenda kwa kiasi gani, hata kama unamhudumia kwa kiasi gani, hawezi tena kudumu na wewe.
Jambo la msingi ambalo unapaswa kuwa nalo makini, ni kuzilinda hisia za mwenzi wako. Kama anakupenda na yupo tayari kwa chochote juu yako, badala ya kufikiria mambo makubwa ya kumfurahisha, anza kwa kitu unachoweza kudhani ni kidogo lakini kina maana kubwa; zilinde hisia zake.
Kulinda hisia za umpendaye, kuna maana pana lakini kwa kifupi, ni kuhakikisha hufanyi mambo ambayo yatamuumiza moyo wake na kumfanya ajute kuwa na wewe. Miongoni mwa mambo hatari kabisa yanayoweza kusambaratisha hisia za kimapenzi, ni usaliti na uongo.
Ukijaribu kufuatilia watu wengi wanaolia na mapenzi, kuna mmoja kati yao amewahi kusaliti au kuwa na viashiria vya usaliti. Kama kweli unampenda na unataka uhusiano wenu hudumu, epuka kabisa usaliti kwenye mapenzi.
Hakikisha mara zote upo kwa ajili yake, hata kama unafanya kazi, tenga muda wa kutosha wa kuwa naye, kaeni pamoja, zungumzeni, pangeni maisha yenu ya baadaye na hakika, utaona jinsi maisha yako ya kimapenzi yanavyokuwa mepesi.
Ukishakuwa na kasumba ya usaliti, mambo mengi yanajifunga. Kwanza hutapenda kuwa unakaa naye karibu, maana utahofia kwamba mkiwa pamoja, mchepuko wako utakupigia simu, utahofia kwamba ataishika simu yako na kusoma meseji mnazowasiliana na michepuko yako.
Ili kuepusha hayo, utakuwa unamkwepakwepa, mara upo bize na kazi, visingizio chungu nzima. Ukaribu ukishaanza kupungua, hata kama hajagundua kwamba unamsaliti, hisia zake zitaanza kuumia ndani kwa ndani na siku akija kugundua, ataunganisha matukio na hisia zake kwako zitaisha kabisa.
Mtu ambaye hisia zake za mapenzi kwako zimeisha, anaweza kukufanyia jambo lolote na hata atakapopata nafasi ya kusonga mbele na maisha yake, utalia na kusaga meno lakini hatakusikiliza wala kukujali tena.
Kwa hiyo badala ya kusubiri mambo yaharibike, ni vizuri ukawa makini kuanzia mwanzo, ziheshimu na zilinde hisia zake. Ukifanya hivi, mapenzi hayawezi kukusumbua.
Tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine.
Comments are closed.