






‘Mtoto mtamu’ katika tasnia ya muziki wa Bongo Fleva, Vanessa Mdee ‘V-Money’ ameshtua na kushangaza wadau na wapenzi wengi wa burudani Bongo, baada ya kuingia mtaani na kuuza CD yenye albamu yake mpya inayojulikana kwa jina la Money Mondays.
Mwanamuziki huyo ambaye kwa sasa anafanya vyema kwenye tasnia ya hiyo, alionekana mapema leo ndani ya Jengo la Mlimani City jijini Dar, akiuza CD hizo, zoezi lililoambatana na upigaji picha wa pamoja na mashabiki zake, jambo lililovuta waengi.
Wakitoa maoni yao juu ya kitendo cha Vanessa kuingia sokoni na kuuza kazi zake mwenyewe, baadhi ya wadau wa muzini waliokuwa eneo hilo wamepongeza na kuwataka wasanii wengine kuiga mfano huo kwani ndiyo njia peke ya karibu ya kuwafikia mashabiki wao.
“Ni jambo jema la kijasiri na linapaswa kuigwa na wasanii wote kwani hii ndiyo njia ya kipekee ya kukutana na mashabiki ambao wanapata fursa ya kueleza matatizo yaliyopo kwenye tasnia ya muziki lakini pia inaepusha wizi wa kazi za wasanii, kwa hiyo Vanessa ameanzisha njia na wengine wafuate,” alisema mmoja wa mashabiki na wadau wa muziki, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu.
Naye kwa upande wake, Vanessa ambaye amejizolea umarufu mkubwa kutokana na ubora wa kazi zake, alisema ameamua kufanya hivyo ili kujiweka karibu na wateja wa kazi zake ikiwa ni pamoja na kuwapunguzia adha za kwenda kutafuta kazi zake mbali na maeneo wanayoishi.
“Hakuna cha ziada bali ni kujiweka karibu na mashabiki zangu ambao kwa kweli bila wao hakuna Vanessa, unajua wakati mwingine hii inaonesha unavyojali watu wako, uwepo wangu hapa Mlimani City tena nikiuza kazi zangu mkononi, kimewavutia wengi na ndiyo maana mmeona namna walivyojitokeza kwa wingi wakitaka kupiga picha na mimi na ninawaomba waniunge mkono kwa kununua kazi zangu orijino,” alisema Vanessa.
NA DENIS MTIMA/GPL
Comments are closed.