WAFANYAKAZI wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam jana walijitolea kufanya usafi katika Hospitali ya Amana ya jijini Dar es Salaam pamoja na kukabidhi vifaa mbalimbali vya kufanyia usafi, ikiwa ni kuadhimisha siku ya usafi duniani zilizofanyika Septemba 21, 2019.
Akizungumza na wanahabari mara baada ya zoezi hilo katika Hospitali ya Amana, Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam na Zanzibar, Bw. Badru Idd alisema zoezi hilo ni utaratibu wa kawaida ambao NMB imejiwekea kuona ni jinsi gani inarudisha sehemu kidogo ya mapato yake katika jamii.
Alisema mbali na zoezi la kufanya usafi hospitalini hapo, wafanyakazi hao walikabidhi vifaa tofauti vya kufanyia usafi vikiwemo vifaa vya kuzolea na kuhifadhia taka, mifagio, vifaa vya kudekia, seti za vifaa vya kujikinga wakati wa kufanya usafi, buti za kufanyia usafi, makoleo maalum ya taka na dawa za usafi.
“Leo tumekuja Hospitali ya Amana kwa ajili ya kujitolea kufanya usafi kuitikia maadhimisho ya usafi duniani, tumejipanga kufanya usafi maeneo mbalimbali ya nchi kwa kuwa tuna mtandao mpana vivyo hivyo wenzetu maeneo mbalimbali wanafanya usafi kama sisi. Na sisi kama kanda ya Dar es Salaam tumeamua kuja kufanya usafi Hospitali ya Amana.”
Akifafanua zaidi alisema NMB pia imekuwa ikitumia fungu hilo katika kusaidia jamii kwenye elimu, afya pamoja na majanga pale yanapojitokeza kwa jamii yetu. “Hii yote ni kuleta ukaribu wa Benki yetu na jamii…hatuji tu kuomba biashara kwa jamii bali tunajitokeza kushiriki, na kusaidiana na jamii katika kufanya shughuli zao. Vifaa vyote tulivyokabidhi leo ni fedha zilizochangwa na wafanyakazi wetu kwa hiyari kujitolea kusaidia jamii,” alisema Bw. Idd.
Aidha aliongeza kuwa NMB wakati wote imekuwa ikishirikiana na jamii katika shughuli mbalimbali, ikiwemo kutenga asilimia moja ya pato lake baada ya kuondoa gharama zote, na kwa mwaka huu imetenga zaidi ya bilioni moja kwa aajili ya shughuli za kijamii, huku hadi kufikia mwezi Julai, 2019 NMB imekwishatumia zaidi ya milioni 450 kwa shughuli kama hizo.
Comments are closed.