SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesisitiza kuwa huduma za uzazi kwa wajawazito zitolewe bila malipo katika hospitali na vituo vya afya vya serikali.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile wakati wa ziara yya kujua hali ya utoaji wa huduma za afya katika Hospitali za Rufaa Temeke, Amana na Mwananyamala leo jijini Dar es Salaam.
Aidha, alisema wanawake wajawazito, watoto chini ya miaka mitano na wazee wasio na uwezo wapate matibabu bure kulingana na sera ya afya inavyosema.
Alisisitiza pia kuwa kila mtoa huduma anapaswa kuandika taarifa ya mgonjwa kabla na baada ya kumpa huduma katika kituo chake cha kazi.
Vilevile, amewataka watoa dawa katika hospitali na vituo vya afya kuandika majina asilia ya dawa na siyo yale ya kampuni na wafuate mwongozo wa dawa uliowekwa na serikali.
“Marufuku watoa dawa kuwaandikia wagonjwa dawa na kwenda kununua nje ya kituo cha afya, badala yake dawa zote zitolewe katika hospitali au kituo cha afya na kama zimeisha zinatakiwa kuagizwa kwa haraka na uongozi,” alisema na kuamuru kwamba wagonjwa wa wodi ya watoto waliokwenda kununua dawa nje warudishiwe fedha zao.
Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa Temeke, Dkt. Amaan Malima, amesema changamoto kubwa inayowakumba ni upungufu wa watumishi.
Wakati huohuo, Mkurugenzi Msaidizi wa Hospitali ya Rufaa ya Amana, Dkt. Meshack Shimwela, aliomba radhi kwa tatizo ambapo wagonjwa walikwenda kujinunulia dawa katika matuka ya nje, akisema hakuna tabia kama hiyo hospitalini hapo na ameahidi kulifanyia kazi haraka iwezekanavyo jambo hilo.
Comments are closed.