Wamiliki, Madereva wa Malori Nchini Watoa Tamko Kufuatia Kushikiliwa kwa Wenzao Zambia
WAMILIKI na madereva wa malori nchini leo wametangaza rasmi azimio lao la kusitisha kupeleka malori yao nchini Zambia na kutoa siku mbili za wenzao wanaoshikiliwa na malori hayo nchini humo kuachiwa vinginevyo watafanya mgomo huo.
Wamiliki hao wamesema madereva hao waliyapakia malori hayo nchini, Congo DRC na kufuata taratibu zote lakini Wazambia wanadai magogo hayo ni mali yao yamepakiwa nchini Zambia kinyume na utaratibu.
Mgogoro huo umechukua karibu miezi minne sasa ambapo imedaiwa mpaka sasa malori na madereva zaidi 480 wanashikiliwa. Wadau hao walizungumza hayo kwenye mkutano na wanahabari uliofanyika Jijini Dar.
Akizungumza kwenye mkutano huo mmoja wa wamiliki wa malori hayo aliyejitambulisha kwa jina la Arold Lema amesema pamoja na kutangaza azimio la kusitisha huduma ya kupeleka malori yao nchini humo wameiomba serikali kuendelea kuwapigania ili wawaokoe wenzao wanaoteseka.
Lema amesema madereva hao wameziacha familia zao kwa kipindi chote hicho jambo linalowafanya waathirike kisaikolojia wao na ndugu zao.
“Baadhi ya madereva hao walioshikiliwa nchini humo wametupigia simu wanaishi mazingira magumu ikiwemo shida ya chakula, maji, matibabu, sehemu za kulala, huduma ya choo na mengineyo.
“Madereva hao wametuambia kutokana na ugumu wa mazingira wanaposhikiliwa wameishiwa pesa hivyo wamekuwa wakiishi kwa kuuza vifaa vya magari yao kama vile matairi, dizeli, spea na vitu vingine alisema Lema.
Pamoja na kuishi katika mazingira hayo madereva hao wamedai kuwa magari yao nayo yamewekwa sehemu yenye vumbi jingi jambo linalohatarisha usalama wa magari hayo.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS NA ISSA MNALLY /GPL