The House of Favourite Newspapers

Wanafunzi wa Kilimo Waula Ufadhili na SBL

0
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) Mark Ocitti (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makamu Mkuu wa chuo cha Kaole Wazazi College of Agriculture kilichopo Bagamoyo Mkoani Pwani, Maximillian Sarakikya (kulia) na mwakilishi wa chuo cha Mt. Maria Goretti College of Agriculture cha Iringa GodfreyKapufi muda mfupi baada ya kutangaza awamu ya pili ya ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa kilimo.

Ikiwa ni muendelezo wa kusaidia sekta ya kilimo hapa nchini, Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) leo imetangaza kuwa itatoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi 30 wa kilimo katika mwaka huu wa fedha (2020/2021).

Idadi hiyo  itafanya jumla ya wanafunzi ambao tayari wameshanufaika na mpango huo wa ufadhili wa masomo kufikia 70 baada ya SBL kutoa ufadhili kwa wanafunzi 40 mwaka wa fedha 2019/2020.

Wanafunzi waliobahatika kupata ufadhili huo kwa sasa wapo vyuoni wakiendelea na masomo.

Ufadhili huu hutolewa na kampuni ya SBL chini ya mpango unaojulikana kama ‘Kilimo-Viwanda Scholarship Program’.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili wa mpango huo ulifanyika jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Mark Ocitti alisema mpango wa kutoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa kilimo unalenga kuisadia Serikali kuwajengea uwezo wa kuzalisha zaidi wakulima kupitia kuwafundishisha wataalamu wa kilimo ambao watawasaidia na kuwashauri.

Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa, SBL imetenga jumla ya TShs milioni 120 ambazo zitatumika kila mwaka kwa ajili kuwalipia wanafunzi wenye sifa na ambao lengo lao ni kusoma masomo ya kilimo na kuongeza kuwa wanufaika watatoka katika familia za wakulima zenye kipato cha chini.

“Ili kutekeleza mpango huu tunashirikiana na vyuo vinne vya ndani ambavyo vinafundisha masomo ya kilimo.

Mkurugenzi Mtendaji wa SBL akisikiliza maswali ya wanahabari (hawapo pichani).

Tunaamini mpango huu utasaidia kuongeza idadi ya wataalamu wa kilimo hapa nchni ambao ni nguzo muhimu ya kuwasaidia wakulima kuongeza uzalishaji wao na mwisho wa vipato vyao,”alisema.

Alisema vyuo ambavyo kampuni hiyo inashirikiana navyo katika utekelezaji wa programu hiyo ni pamoja na Kaole Wazazi College of Agriculture kilichopo Bagamoyo Mkoani Pwani, Kilacha Agriculture and Livestock Training Center kilichopo Moshi, Mt. Maria Goretti College of Agriculture cha Iringa pamoja na Igabiro Training Institute of Agriculture kilichopo Bukoba, mkoani Kagera.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wakuu wenzake wa vyuo vinavyonufaika na mpango huo, Mkuu wa Chuo cha Kilacha Agriculture and Livestock Training Center Benito Mwenda aliishukuru kampuni ya SBL kwa kuja na wazo la kutoa ufadhili wa masomo ya kilimo na kuongeza kuwa ili kilimo kiweze kuwa chenye tija wataalamu wengi wanahitajika.

“Tunayo furaha kwa kuwa ufadhili huu unawalenga wanafunzi wanaotokea katika familia zenye vipato duni ambao kama siyo msaada wa SBL, wasingeweza kupata fursa ya kusoma na kubadilisha maisha yao pamoja na ya jamii zao,” alimaliza kusema Ocitti.

Leave A Reply