WATOTO, VIJANA WAFUNDISHWA KUJIWEKEA AKIBA
WAZIRI wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amewataka wazazi kuweka utaratibu wa kuwawekea watoto wao akiba ya fedha katika akaunti ya Wajibu ya benki ya NMB, kwa ajili ya matumizi ya baadaye.
Ummy aliyasema hayo wakati akizindua kampeni ya uhamasishaji wa elimu ya utunzaji wa fedha inayojulikana kama Jifunze, Jipange, Wajibika iliyoanzishwa na benki hiyo.
Waziri huyo alisema wazazi na walezi wengi wamekuwa wakitumia pesa nyingi katika mambo ambayo hayana umuhimu mkubwa na hivyo kusahau kuweka akiba ya watoto wao ambapo akiba hiyo ingeweza kuwasaidia kwa matumizi ya baadaye.
“Nimefurahi NMB mmeamua kwenda kufunza watoto WAJIBIKA, tatizo Watanzania kwenye matumizi yetu hayana kipaumbele kama mfano kutuza fedha watu katika burudani mbalimbali ambapo watu hutoa pesa nyingi lakini hawawawekei watoto akiba katika mabenki.
“Ujumbe wangu kwa Watanzania ni kwamba hela ambayo unaitumia kwa matumizi yasiyo ya lazima, tenga angalau kiasi kidogo kwa ajili ya mtoto wako,” alisema.
Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Ineke Bussemaker, alisema NMB inatambua umuhimu kwa watoto kujua ulazima wa kujiwekea akiba, hivyo ilianzisha kampeni hiyo ili kuwasaidia watoto kupata elimu ambayo wanaamini kwamba wakielimishwa , itawasaidia kwa miaka ijayo kuwa na kizazi ambacho kitakuwa kinaweka akiba ya baadaye.
Comments are closed.