The House of Favourite Newspapers

Waziri Dkt. Gwajima Akutana Na Mwakilishi Mkaazi Un Women

0
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima(kulia) akipokea zawadi ya kanga kutoka kwa Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya wanawake (UNWOMEN) Hodan Addouh,(kushoto) ofisini kwake Dodoma.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na taasisi za kimataifa zinazojihusisha na masuala ya uwezeshaji wa wanawake kiuchumi kwa lengo kuchochea usawa wa kijinsia nchini.

 

Waziri Dorothy Gwajima amesema hayo Jijini Dodoma alipofanya mazungumzo na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa UNWOMEN Hodan Addou aliyefika Ofisini kwake kwa ajili ya kujitambulisha.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akipokea (kushoto) zawadi kutoka kwa Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya wanawake (UNWOMEN) Hodan Addouh, ofisini za Wizara Dodoma kulia akishuhudia ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima.

Amesema Tanzania inaendeleza jitihada zake za kumkomboa mwanamke katika nyanja zote za maendeleo na itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo likiwemo Shirika la UNWOMEN ambalo limekuwa na mchango mkubwa katika kuchagiza mipango ya maendeleo kwa wanawake.

 

“Tanzania inazingatia masuala ya usawa wa kijinsia kwa sababu kwenye Ilani yetu yametajwa namna kumfanya mwanamke wa Kitanzania anakua kiuchumi, lazima tumuendeleze” amesema Dkt. Gwajima.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima (kushoto) akizungumza na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya wanawake (UNWOMEN) Hodan Addouh, (kulia) ofisini kwake Dodoma katikati ni Naibu wake Dkt. Godwin Mollel.

Ameongeza kuwa, Serikali ya awamu ya tano chini uongozi wa Rais John Magufuli imetekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya kuwawezesha wanawake katika nafasi mbalimbali za uongozi.

 

Amefafanua kuwa msaada wa mashirika kama UNWOMEN katika kuwawezesha wanawake kwenye masuala ya uongozi, uwezeshaji kiuchumi, Tanzania ilishatoa kipaumbele kufanikisha masuala hayo.

 

Naye Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel amemshukuru Hodan kwa kuendeleza ushirikiano na Tanzania na kuhimiza wanaume kushirikishwa katika program za ukombozi wa wanawake.

 

Amesema misingi iliyokitwa katika mazingira ya unyanyasaji wa wanawake siku zote inaongozwa na kusimamiwa na wanaume kwa hiyo kuna umuhimu wa kuwa kuwashirikisha wanaume katika mapambano dhidi ya ukatili.

 

Dkt. Mollel amesema kwa kawaida tangu zamani ni muhimu kwa wanaume kuwapenda wanawake kutokana na mchango wao katika maendeleo ya familia kwa ujumla na Mwanaume asiyependa mwanamke hana ndoto ya kufikia maendele endelevu.

 

“Wazee wetu walikuwa wakitueleza, mwanaume asiyependa mwanamke hapendi maendeleo” alisema na kuongeza kuwa umefika wakati kwa wanaume kushirikiana na wenzi wao wanawake kujenga misingi ya uchumi imara.

Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi Hodan amesema UNWOMEN inajivunia kushirikiana na Tanzania kwa sababu ina miongozo ya kuwawezesha wanawake kushiriki katika sekta zote ikiwemo uongozi.

 

Amesema kuwa UNWOMEN imekuwa ikitekeleza mipango ya kipaumbele ya Serikali katika kuchochea maendeleo hususan ya wanawake katika uongozi, Uwezeshaji wa wanawake kiuchumi, kuandaa na kuweka mipango mkakati na kuandaa bajeti yanye mrengo wa kijinsia.

 

Ametaja maeneo ya kipaumbele katika kuwawezesha wanawake kuwa ni pamoja na upatikanaji wa nishati ya umeme, maji safi na miundombinu ya Barabara ili kuhakikisha vikwazo vya maendeleo ya wanawake vinatoweka.

 

UNWOMEN imetenga zaidi ya dola za Kimarekani 570,000 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kumwezesha Mwanamke katika nyanja mbalimbali.

Na Mwandishi Wetu Dodoma

 

Leave A Reply