Yanga Yagomea Mechi Yao Kuahirishwa
BODI ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imeahirisha mechi mbili za Ligi Kuu ya Tanzania Bara zinazozihusu Klabu za Simba na Yanga ili kuzipa nafasi timu hizo kujiandaa na pambano la watani wa jadi.
Watani hao wa jadi wanatarajiwa kuvaana Septemba 30, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam mchezo unaotarajiwa kujaa upinzani mkubwa.
Maamuzi hayo ya bodi yamechulikuwa tofauti na mashabiki wa Yanga ambao wameonekana kugomea michezo hiyo kuahirishwa wakidai wanawabeba watani wao, Simba ambao wamepata matokeo mabaya kwenye michezo miwili mfululizo ya ligi.
Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumamosi, kutoka kwenye bodi hiyo ilisema mechi hizo ni Yanga dhidi ya JKT Tanzania na Simba SC dhidi ya Biashara United zilizopangwa kufanyika Septemba 25 na 26 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar.
Baada ya mchezo huo kusogezwa mbele, timu hizo za Simba na Yanga zitacheza michezo yao ya mwisho ya ligi wikiendi hii ambako Simba watacheza na Mwadui FC kesho Jumapili saa kumi kamili Uwanja wa Kambarage, Shinyanga.
Yanga wenyewe watajitupa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar saa moja kamili usiku kukipiga na Singida United mchezo ambao wanahitaji ushindi ili warejee kileleni.
Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumamosi, kutoka ndani ya uongozi wa Yanga, wenyewe wamekataa mchezo wao na JKT Tanzania kuahirishwa na badala yake waendelee kama kawaida.
“Wao kama wanataka kutuliza presha iliyokuwepo Simba baada ya kupata matokeo mabaya ya mechi zao mbili walizozicheza waseme tu, lakini siyo kuleta sababu ya maandalizi ya mchezo wa Simba na Yanga.
“Inamaana hao Bodi ya Ligi hawajaona wakati wanapanga ratiba ya mechi ya Simba na Yanga hadi leo hii waibuke na kutaka kusogeza mbele mchezo wetu wa watani wa jadi?” Alihoji mtoa taarifa huyo.
Alipotafutwa Ofisa Habari wa Yanga, Dismas Ten kuzungumzia suala hilo simu yake iliita bila ya kupokelewa.
Hata hivyo, Kocha Mkuu wa Yanga Mkongomani, Mwinyi Zahera hivi karibuni alisema kuwa anataka kushinda michezo miwili iliyokuwepo mbele yake dhidi ya Singida na JKT Tanzania kabla ya kukutana na Simba.
Kwa upande wa Simba, Championi Jumamosi lilimtafuta, Ofisa habari wake, Haji Manara ambapo naye simu yake iliita bila kupokelewa.
Stori na Wilbert Molandi na Musa Mateja
Comments are closed.