The House of Favourite Newspapers

Zahera: Nashusha Mgabon

KOCHA Mkuu wa Yanga Mkongomani, Mwinyi Zahera amesema kuwa tayari amefikia muafaka mzuri na straika Mghana, kiungo kutoka Gabon, winga Mkongo na beki ambaye ameficha nchi anayotokea na jina lake.

 

Hiyo, yote katika kukiimarisha kikosi chake ili kifanye vizuri katika Ligi Kuu Bara inayoendelea ambayo hadi hivi sasa tayari imecheza michezo tisa huku ikifikisha pointi 25 ikiwa nafasi ya pili katika msimamo wa ligi.

 

Usajili wa dirisha dogo unatarajiwa kufunguliwa Novemba 15, mwaka huu kwa wachezaji huku kocha huyo mwenye uraia wa nchi mbili wa DR Congo na Ufaransa akipanga kukabidhi ripoti hiyo ya usajili hivi karibuni.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Zahera alisema wachezaji hao wanne wanatarajiwa kutua nchini wakati wowote na kikubwa kinachosubiria ni tiketi pekee za ndege ambazo kama wakitumiwa, basi wanatua.

 

Zahera alisema, kiungo wa Gabon yeye alikuwa na mkataba na klabu yake ya nchini huko aliyokuwa anaichezea ambao umemalizika mwishoni mwa mwezi uliopita, hivyo atatua kama mchezaji huru.

 

Aliongeza kuwa, kikubwa kitakachowazuia wachezaji hao ni dau la usajili pekee, lakini kwa maana mazungumzo yamekwenda vizuri baada ya kufanikiwa kuwashawishi na kukubali kuja kuichezea Yanga.

 

“Ninafahamu kila timu itafanya usajili katika dirisha dogo na mimi nimepanga kukiboresha kikosi changu kwa kusajili wachezaji kulingana na upungufu wa baadhi ya sehemu kama kiungo, beki, mshambuliaji na winga.

 

“Na tayari nimeshalimaliza hilo binafsi kwa kufanya mazungumzo na wachezaji baadhi ambao ni Mghana anayecheza nafasi ya ushambuliaji, kiungo kutoka Gabon, winga Mkongo na beki yeye nitamtangaza baada ya kumalizana naye tupo katika hatua nzuri.

 

“Ninaamini kama tukifanikiwa kuwasajili wachezaji hao wote, basi ninaahidi timu yangu kufanya vizuri zaidi hivi tunavyoendelea katika ligi, niwatoe hofu mashabiki wa Yanga mazungumzo yanakwenda vizuri,” alisema Zahera.

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.