The House of Favourite Newspapers

Kocha Mserbia Kumrithi Mbelgiji Simba

LICHA ya kuondoka kimyakimya, lakini Spoti Xtra limebaini kwamba Kocha wa Simba, Patrick Aussems yupo Afrika Kusini kukamilisha dili lake na Klabu ya Polokwane na muda wowote ujumbe wa kushtua unaweza kuonekana kwenye akaunti yake ya Twitter au Instagram.

 

Lakini Simba nao ni wajanja kwelikweli, wameshalisoma picha lote kimyakimya na wamemvutia waya Kocha Mserbia, Goran Kopunovic na kumwambia akae mkao wa safari.

Aussems aliondoka Dar es Salaam kimyakimya mapema wiki hii, huku Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Senzo Mazingisa akikiri anajua kocha huyo hayupo ila hajui amekwenda wapi.

Mbelgiji huyo inadaiwa aliomba ruhusa ya siku mbili ya kufanya ishu zake, ili arejee kuwahi mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Ruvu Shooting Jumamosi kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar.

 

Lakini Habari za uhakika ambazo Spoti Xtra limezipata ndani ya Simba na vyanzo vingine nchini Afrika Kusini ni kwamba, Aussems anafanya siri kubwa lakini anakamilisha dili lake na Polokwane ambayo imetimua Kocha Mserbia, Zlatko Krmpotic.

Krmpotic alipigwa mechi tano mfululizo, Polokwane wakamuonyesha mlango wa kutokea na kumpigia simu Aussems fasta.

 

Habari zinasema kwamba Polokwane wanataka kama itawezekana Aussems awe kwenye benchi lao kwenye mechi dhidi ya Orlando Pirates Jumanne ijayo kuokoa jahazi kwani hali ni mbaya.

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa benchi la ufundi lilianza kuingia hofu juu ya safari ya Aussems kwenda na kurudi Ubelgiji kwa kutumia siku mbili kitu ambacho siyo cha kawaida huku wakipata taarifa kutoka kwa mmoja wa rafiki wa karibu wa timu hiyo amekwenda kwenye moja ya nchi ya Afrika kukamilisha dili hilo.

 

Habari zinasema kwamba Aussems aliamua kujiongeza na kudaka dau nono la Polokwane baada ya kunusa tetesi kwamba ajira yake iko matatani na muda wowote angeweza kupigwa chini Msimbazi.

Inadaiwa kwamba licha ya kumpa matumaini lakini Simba hawaridhishwi na kiwango cha soka la timu hiyo msimu huu ikiwa ni kuanzia itolewe kimataifa huku ikidaiwa wachezaji wengi hawatumiki ipasavyo.

 

GORAN ANARUDI

Kocha huyo Mserbia aliyewahi kuinoa Simba akaondolewa kimizengwe msimu wa 2014/15, amepigiwa simu na viongozi na anapewa nafasi kubwa ya kurejea Msimbazi muda wowote ambao Aussems atatema mzigo.

 

“Hata kabla hajaondoka viongozi walishazungumza na Goran na muda wowote utasikia ametua, viongozi wanaamini ana uwezo mkubwa na kwa mashindano tunayoshiriki anayamudu kabisa na Simba ikacheza kiwango cha juu,” alisema kiongozi mmoja ndani ya Simba.

Alidokeza kwamba kuna baadhi walikuwa wanapendekeza Mkongomani aliyetimuliwa na Yanga, Mwinyi Zahera apewe kazi ya muda lakini wengi wakapinga haraka sana kwa madai kwamba hafai na ana mdomo sana.

 

“Zahera alitajwa lakini wengi walimkataa haraka sana wakasema hana kiwango cha Simba na anapenda sana maneno kuliko kazi, huku wakirejea alivyowapaka Yanga baada ya kutemwa,” aliongeza mtoa habari wetu ambaye yuko ndani ya Simba muda mrefu.

Simba inapambana kubeba taji la Ligi Kuu Bara na kurejea kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika Msimu ujao.

WILBERT MOLANDI NA SAID ALLY, Dar es Salaam

Comments are closed.