The House of Favourite Newspapers

Njemba aua wawili na kujeruhi Sita

20170122_081935

Wakazi na wafanyabiashara wa Mabibo jijini Dar es Salaam wakiwa wameizunguka ofisi ya soko la Mabibo-Mwisho alimohifadhiwa mtu anayetuhumiwa kuua na kujeruhi watu kadhaa katika soko hilo kabla polisi hawajafika.

DAR ES SALAAM: Inatisha! Njemba mmoja, Shadra Maninje ‘Idd’, anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kuwaua watu wawili na kujeruhi wengine wanne kwa kuwachoma visu sehemu tofauti za miili yao akiwemo mtoto wa kike, Fatuma Hamis mwenye umri wa miaka miwili.

 nit

Jengo la Mapokezi chuo Cha Taifa cha Usafirishaji (NIT)

TUKIO hilo lililozua tafrani kwa wakazi wa Mtaa wa Jitegemee, maeneo ya Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Mabibo jijini Dar, lilijiri usiku wa kuamkia jana ambapo ilidaiwa kuwa Idd alikuwa amelewa na kila aliyekuwa anakutana naye alikuwa akimshambulia kwa kisu.

Wakizungumza na Wikienda lililofika eneo la tukio, kila shuhuda alikuwa na lake la kusema kutokana na mshangao walioupata.

“Hatujui nini kilimpata Idd kwani alionekana amelewa na alipokuwa anakutana na mtu anamchomachoma visu. Alimchoma Miraji Kondoa kisu cha kifuani na kufariki dunia.

“Pia inasemekana kuna mwanachuo wa NIT wa kike alimchoma kisu na yeye alifariki dunia.

“Mbali na hao alimchoma kisu mfanyabiashara aliyefahamika kwa jina la Jackson Mushi ‘Rasta’ sehemu ya tumboni na utumbo kuonekana. Baadaye wasamaria walimpeleka Hospitali ya Mwananyamala.

“Baada ya kufanya matukio hayo, watu walianza kumkimbiza huku wakiwa wameshika mawe. Alipoona hivyo alikimbia na kupotelea uchochoroni lakini cha ajabu alipofika huko nako alimchoma kisu mwanafunzi wa NIT,” alisema mmoja wa mashuhuda huyo akiungwa mkono na mwingine:

“Mbali na huyo kuna mama mwingine ambaye hajafahamika naye alichomwa kisu cha tumboni na kutokezea mgongoni na inasemekana hali yake ni mbaya sana.”

Katika tukio hilo, wanahabari wetu walizungumza na mmoja wa majeruhi ambaye ni mwanafunzi wa NIT, Maiko Erasto (26) ambapo alisimulia:

“Nilikuwa ndani na mwenzangu, ghafla tulisikia kishindo cha kitu kuanguka nje, nikatoka ili kufahamu kilichotokea, nilipofungua mlango nikamuona jamaa ambaye sikuwa namfahamu, akanyanyua kisu kunichoma kichwani nikakwepa lakini kikanipata begani.

“Baada ya kuona vile, mwenzangu alinivuta chumbani na kuufunga mlango, kumbe pale nje kulikuwa na mtoto wa kike (Fatuma Hamis) ambaye naye alichomwa kisu shingoni na ameshonwa nyuzi 8.”

Naye Mwenyekiti wa Mtaa wa Jitegemee,  Kilema alikiri kutokea kwa tukio hilo la kusikitisha na kusema kuwa kuna watu walipoteza maisha na wengine kujeruhiwa na mtuhumiwa huyo ambaye alikamatwa na kufikishwa katika Kituo cha Polisi cha Urafiki jijini Dar.

 20170122_0819380

Wakazi na wafanyabiashara wa Mabibo jijini Dar es Salaam wakiwa wameizunguka ofisi ya soko la Mabibo-Mwisho alimohifadhiwa mtu anayetuhumiwa kuua na kujeruhi watu kadhaa katika soko hilo kabla polisi hawajafika.

Richard Bukos, Issa Mnally, Salum Milongo na Gabriel Ng’osha/GPL

 

 

 

Comments are closed.