The House of Favourite Newspapers

Rais Magufuli Asisitiza Kuhamia Dodoma

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 16 Machi, 2017 ametembelea eneo la ujenzi wa Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma na kuwahakikishia wananchi kuwa atahamia Dodoma hivi karibuni kama alivyoahidi.
Mhe. Rais Magufuli ambaye ameongozana na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenister Joakim Mhagama na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi amesema pamoja na majengo ya Ikulu Serikali itajenga miundombinu mingine zikiwemo reli na barabara za lami zitakazounganisha maeneo ya vijiji vinavyozunguka Ikulu na mji wa Serikali.
Pia Mhe. Dkt. Magufuli amewahakikishia wananchi kuwa wote watakaoguswa na shughuli za ujenzi wa miundombinu ya Serikali na wanaostahili kulipwa fidia watalipwa, na ametoa wito kwa wananchi hao kutumia fedha za fidia watakazolipwa kujenga makazi bora na kujipanga kufanya shughuli zenye manufaa kwao.
“Hapa sasa watakuja watu wengi, wafanyakazi na wageni maana tayari Mabalozi wa nchi mbalimbali nao watajenga ofisi zao hapa, sasa na nyinyi mjipange kufanya biashara, mtapata soko la kuuza mazao na bidhaa nyingine, mkipata fedha ziwasaidie kwa manufaa na sio kuzichezea” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
Kwa upande wake Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa amesema utekelezaji wa Serikali kuhamia Dodoma unakwenda vizuri ambapo mpaka sasa viongozi wakuu wa wizara zote na wafanyakazi 2,069 wameshahamia Dodoma na wengine wanaendelea kuhamia Dodoma.
Mhe. Majaliwa ameongeza kuwa atasimamia utekelezaji wa maagizo ya Mhe. Rais Magufuli aliyeagiza kujengwa kwa reli itakayounganisha eneo la Bwigili na Dodoma mjini ili kurahisisha usafiri wa watu pamoja na kuharakisha ujenzi wa barabara za kuzunguka mji wa Dodoma na barabara za kuunganisha mji wa Serikali na Dodoma Mjini.
Wakiwa katika eneo hilo, Mhe. Rais Magufuli na Waziri Mkuu Mhe. Majaliwa wameshiriki ufyatuaji wa matofali yatakayotumia katika ujenzi wa majengo ya Ikulu.
Mapema kabla ya kutembelea eneo hilo, Mhe. Rais Magufuli amepokea taarifa ya mapendekezo ya ujenzi wa Mji wa Serikali wa Makao Makuu Dodoma kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Mhandisi Paskasi Muragili na kuagiza ujenzi wa Mji huo uzingatie maslai ya Taifa.

Comments are closed.