DAR ES SALAMA: Mwili wa aliyekuwa kiongozi wa Jumuiya ya Freemason Afrika Mashariki, Sir Jayantilal Andy Chande, aliyefariki Aprili 7, mwaka huu nchini Kenya, umezikwa kwa kuchomwa moto jana hadi kubaki jivu katika Makaburi ya Baniani, yaliyopo Makumbusho jijini Dar.
Baadhi ya viongozi wastaafu waliohudhuria mazishi hayo ni pamoja na Mawaziri Wakuu, Mzee Cleopa David Msuya na Jaji Joseph Warioba na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Juma Mwapachu.
Mamia ya waombolezaji walianza kukusanyika makaburini hapo kuanzia saa nne asubuhi wakiusubiri mwili wa marehemu uliokuwa ukifanyiwa maombi ya mwisho nyumbani kwake, Oysterbay. Saa 5 asubuhi, mwili huo uliwasili eneo la makaburini ukiwa umewekwa juu ya machela na kubebwa mabegani na wanaume waliovalia mavazi meupe huku watoto wake Rupen, Manish, Anoj wakiwa mbele ya msafara.
Baada ya kufikishwa mbele ya Mungu wa Baniani (Ram) na kufanyiwa maombi mafupi, uliwekwa kwenye tanuru lililopangwa magogo ambalo lipo ndani ya jengo kubwa makaburini hapo na kumwagiwa mafuta ya samli.
Watoto watatu wa marehemu waliuzunguka mwili wa baba yao uliokuwa kwenye magogo huku mikononi wakiwa wamekamata kigingi cha moto, ambapo kabla ya kuyawasha, waliuzunguka mara nne.
Mmoja wa watoto wa marehemu, Manish Andy Chande, aliliambia Risasi Mchanganyiko kuwa kifo cha baba yao kimeacha pengo lisilozibika.
Mzee Chande, ambaye amewahi kufanya kazi katika idara mbalimbali za umma tangu enzi za Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, amefariki akiacha mke, watoto watatu na wajukuu watatu, akiwa na umri wa miaka 88.