Baada ya Kutolewa Caf, Sasa Yanga Kumalizia Hasira Kwa Prisons leo, Taifa
Timu ya Yanga inatarajiwa kushuka uwanjani leo Jumamosi saa kumi kamili kukipiga dhidi ya Tanzania Prisons katika mechi yao ya Robo Fainali ya Kombe la Shirikisho, maarufu kama Kombe la FA.
Mchezo huo utakaopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar, unatarajiwa kuwa mgumu kwa kuwa timu zote ni za Ligi Kuu Tanzania Bara ambapo bingwa wa michuano hiyo anapata nafasi ya kushiriki katika Kombe la Shirikisho Afrika msimu ujao.
Yanga itaingia uwanjani kwa mara ya kwanza tangu ilipotolewa katika michuano ya Kombe la Shirikisho (CAF), wiki iliyopita.
Kocha Msaidizi wa Yanga, Juma Mwambusi ameshaweka wazi kuwa hawatawadharau Prisons na kudai kuwa ushindi ndiyo kitu muhimu kwao na wataingia wakiwa na nguvu kubwa.
Jana Ijumaa asubuhi Yanga iliutumia Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kufanya mazoezi kujiandaa na mchezo huo
Upande wa Kocha wa Prisons, Mohammed Abdallah alitamba kupata ushindi akisema: “Yanga ni timu kama zilivyo timu nyingine na imeshiriki michuano mikubwa ya kimataifa mara nyingi.”
Kabla ya kufika hatua hiyo, Prisons iliitoa Mbeya City wakati Yanga iliitoa Kiluvya United ya Pwani.