KIKOSI cha Yanga hivi karibuni kinatarajia kuingia kambini kuanza kujiandaa kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Bara ambapo kwa sasa kinachokwamisha kuanza kwa kambi hiyo ni kocha wao mkuu, George Lwandamina raia wa Zambia ambaye bado hajarejea nchini.
Lwandamina aliyeipa ubingwa wa ligi Yanga msimu uliopita bado hajarejea nchini kutokana na kuwepo nchini kwao akimalizia mapumziko yake baada ya kumalizika kwa ligi.
Akizungumza kupitia Kipindi cha Spoti Hausi kinachorushwa na GlobalTv Online, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari cha Yanga, Godlisten Anderson ‘Chicharito’ amesema kuwa kikosi hicho kimepanga kuanza kambi yake kuanzia Julai 2 au 3, mwaka huu ambapo kambi hiyo itategemea na mawazo ya kocha huyo.
“Kinachotusubirisha kuanza kambi yetu ni kocha Lwandamina ambaye bado hajarejea nchini kutoka kwao Zambia alipoenda kwa ajili ya mapumziko tangu ligi ilipomalizika, lakini tunategemea hivi karibuni atarejea na tutaanza kambi yetu.
“Kambi rasmi inaweza kuwa Julai 2 au 3, ila hatujajua ni wapi ambapo tutaenda kuweka kambi hiyo mpaka kocha aje na kusema wapi twende japo kuna maeneo sita ambapo pamependekezwa kwenda kuweka kambi,” alisema.