The House of Favourite Newspapers

Chirwa Aibuka Achimba Mkwara Mzito

0

MUDA mfupi baada ya Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kusema straika wa Yanga, Obrey Chirwa, hana hatia na yupo huru kuitumikia timu yake, mchezaji huyo amezipiga mkwara timu pinzani.

Juzi Alhamisi, kamati hiyo ilisema Chirwa na Deus Kaseke ambaye alikuwa Yanga kabla ya kwenda Singida United, hawana hatia baada ya hapo awali kutuhumiwa kumwangusha mwamuzi, Charles Ludovic.

 

Wawili hao walituhumiwa kutenda kosa hilo katika mechi yao ya mwisho ya Ligi Kuu Bara msimu uliopita dhidi ya Mbao FC kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza ambapo Yanga ilifungwa bao 1-0.

Msuva pekee ndiye aliyekutwa na hatia na amepewa onyo kali. Hata hivyo, kwa sasa Msuva anaichezea Difaa Al Jadida ya Morocco.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Chirwa alisema: “Hata kama ningefungiwa kucheza mechi kadhaa za ligi kuu, naamini wachezaji waliopo wangepambana na kuipa matokeo mazuri timu yangu.

 

“Kwa sasa mimi bado ni majeruhi, lakini siku si nyingi nitarudi uwanjani kuendeleza mapambano waliyoyaanzisha wenzangu katika kutetea ubingwa wetu wa msimu uliopita.

 

“Nikirudi uwanjani mashabiki wategemee kuuona moto wangu ule wa siku zote na sasa nitapambana sana kuhakikisha timu yangu inatetea ubingwa kwa mara nyingine kwani tuna kikosi kizuri na cha ushindani,” alisema Chirwa.

 

Chirwa ambaye anasumbuliwa na goti, msimu uliopita alifunga mabao 12 katika Ligi Kuu Bara huku akiibuka Mfungaji Bora wa Kombe la FA akiwa amefunga mabao sita.

NAFASI 45 ZA KAZI KUTOKA WILAYA YA KIBITI

Leave A Reply