The House of Favourite Newspapers

Daktari Amruhusu Ngoma Kuwavaa Waethiopia

Mshambuliaji wao Donald Ngoma (wa pili kutoka kulia).

DAKTARI Mkuu wa Yanga, Edward Bavu amemruhusu mshambuliaji wao Donald Ngoma kucheza dhidi ya Wolayta Dicha ya Ethiopia kwa kumuanzishia programu ya kuuchezea mpira kama sehemu ya maandalizi ya mechi hiyo ya Kombe la Shirikisho Afrika.

 

Ngoma amerejea uwanjani akitokea kwenye majeraha ya nyonga aliyoyapata tangu Agosti, mwaka jana kutokana na tatizo hilo na kulazimika kukaa nje ya uwanja akiuguza maumivu hayo.

 

Yanga kwenye Kombe la Shirikisho Afrika inavaana na Wolayta baada ya droo kuchezeshwa na mchezo wa kwanza utapigwa Aprili 6-8 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Bavu alisema Ngoma ataanza mazoezi hayo ya kuchezea mpira baada ya kumaliza programu ya mazoezi ya binafsi ya peke yake ya kukimbia mbio fupi na ndefu.

 

Bavu alisema, mshambuliaji huyo tayari amemaliza programu hiyo na Jumatatu ijayo asubuhi ataanza mazoezi magumu na wenzake ikiwemo kuchezea mpira akijiandaa na mchezo wa kimataifa.

 

“Kila mazoezi aliyokuwa akiyafanya Ngoma yalikuwa na programu yake na tayari amemaliza programu yake ya mazoezi ya binafsi ya kukimbia mbio fupi na ndefu baada ya kumzuia kuchezea mpira.

 

“Hivi sasa tayari amemaliza programu hizo na Jumatatu ataanza programu ya kuchezea mpira pamoja na wenzake katika mazoezi ya kujiandaa na mechi na Waethiopia.

 

“Nilimpa programu hizo baada ya kuhofia kujitonesha kama unavyojua ametoka kwenye majeraha makubwa na alikaa nje muda mrefu ni lazima aanze taratibu,” alisema Bavu.

Stori: Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.