The House of Favourite Newspapers

Mashabiki Inabidi Muelewe, Hakuna Uchawi Kwenye Soka

BADO mchezo wa Simba na Yanga ul­iochezwa Jumapili iliyopita unaende­lea kuwa gumzo kutokana na matukio kadhaa yaliyojitokeza kwenye mchezo huo. Matokeo ya mchezo huo yalikuwa ni 0-0.

 

Kitendo cha kwanza tu kili­chofanywa na mshambuliaji wa Yanga, Ibrahim Ajibu cha kuu­piga mpira nje baada ya filimbi ya kuanzisha mpira kupulizwa, ndicho kimekuwa gumzo kubwa.

 

Wengi wamekuwa wakihoji juu ya suala hilo na kulihusi­sha na masuala ya kishirikina kitu ambacho naona hakina maana yoyote mbaya. Niwaam­bie tu mashabiki wa soka kuwa, kwenye mchezo huu usiamini sana uchawi.

 

Kitaalamu mchezaji akiwa uwanjani anatambua majuku­mu yake ipasavyo, pia anatam­bua jinsi kikosi chake kilivyo hasa kikiwa na mpira ama kikipoteza mpira, hivyo jambo la msingi kabisa ni kujipanga upya pale ambapo anadhani kikosi chake hakipo sawa.

Mwalimu naye ana nafasi yake katika kutoa maelekezo, hivyo mbinu zake ndizo am­bazo hutumika siku zote uwan­jani na ndio maana wachezaji wengi ambao walisajiliwa kwa maelekezo ya mwalimu hufan­ya vizuri ndani ya kikosi kwa kuwa lilikuwa ni hitaji lake.

 

Sasa kitu cha kushangaza kama kulikuwa na uchawi kuto­kana na lile tukio, kwa nini hawakushinda! Tuache imani potofu.

Kila mmoja sasa amekuwa mchambuzi na anaeleza kile ambacho anafikiria ni sahihi hasa katika mpira wa miguu jambo ambalo si sawa na kama litaendelea kuzungumzwa mara kwa mara linadumisha maendeleo ya soka letu.

 

Muda umefika sasa wa kuwa na ligi yenye ushindani ambao tunaufikiria siku zote jambo ambalo litadhihirisha kwamba tunaweza kuwa na timu ya taifa bora na yenye ushindani kwa kuwa ligi ipo vizuri.

 

Mambo yalivyo kwenye soka huwezi kutabiri na ndio maana wengi wanashindwa kuelewa kwamba kama mpinzani aki­fanikiwa kuziba njia za mpira inakuwa ngumu kwa mshindani wake kuweza kupenya katika ngome ya mwenzake.

 

Ipo wazi kwamba kuna mechi kadhaa ambazo Simba imefani­kiwa kucheza vizuri na kupata ushindi hasa ukiangalia mch­ezo wao wa kwanza dhidi ya Prisons walishinda, pia katika mchezo dhidi ya Mbeya City waliibuka na ushindi, lakini ika­toka suluhu na Ndanda kabla ya kupoteza mbele ya Mbao FC na kuja kupata ushindi kwa Mwadui.

 

Je nafasi ya uchawi katika mechi hizi ambazo Simba haik­ufanya vizuri upo wapi ama ndio tunatafuta sababu ya kushindwa ili tuweze kuwahar­ibu kisaikolojia wachezaji wetu. Muda huo haupo tena kwa sasa kila mmoja apambane kuhak­ikisha kwamba timu yake ina­fanya vizuri.

 

Usajili mzuri sio sababu ya kuweza kukupa ushindi bali ni mbinu ambazo unazitumia ni rafiki katika kushindana kwako kwa wakati huo na je kila mchezaji anatimiza wajibu wake ipasavyo?

 

Kama kila mmoja anapam­bana basi huo ndio ushindani wenyewe na tunataka uwe hivyo katika kila mchezo am­bao utachezwa kwenye ligi msimu huu.

Kila siku tumekuwa tukipiga kelele juu ya timu kuonyesha ushindani kitu ambacho ki­narudishwa nyuma na suala la kukosekana kwa mdhamini mkuu katika ligi hiyo.

 

Imani yangu ni kwamba kama kungekuwa na mdhamini mkuu katika ligi kuu msimu huu, tungeshuhudia ushindani usio wa kawaida hata kombe nalo lingeenda kwa timu am­bayo haijatarajiwa.

 

Lakini kama ambavyo mnajua kwamba katika ligi yetu hii timu zenye fedha ambazo zinajiweza kwa kila kitu, ndizo huwa na nafasi kubwa ya kufanya vizuri.

 

Kwa mwendo huo kila msimu tutakuwa tukishuhudia timu zilezile zikiwa juu ya msimamo na kubadilishana katika kutwaa ubingwa.

MAKALA NA MOHAMMED HUSSEIN

Comments are closed.