The House of Favourite Newspapers

Mambo 5 Lowassa akianguka

0

Na Mwandishi Wetu
WAKATI siku 32 zikiwa mbele kuufikia uchaguzi mkuu Oktoba 25, mwaka huu, tegemeo kuu la mgombea urais wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa ni kutokea kwa mambo matano endapo ataanguka kwenye kinyang’anyiro hicho, Uwazi limechimba.

 Mgombea urais wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Edward Lowassa.

Kwa mujibu wa mchambuzi mmoja wa mambo ya siasa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ‘Mlimani’, Profesa Nathaniel Mlaumi, Lowassa ana siku chache za maamuzi mengine endapo ataangushwa kwenye mbio za urais na mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), John Magufuli.

MOJA

“Kwanza, kila mtu anajua kwamba, Ukawa una nguvu na umepata nguvu zaidi baada ya Lowassa kuingia Chadema na wafuasi wengi.“Kama Lowassa atashindwa kwenye uchaguzi Oktoba, hata Ukawa itasambaratika. Haitakuwepo tena na maana ya Ukawa itakomea hapo. Naamini kama Lowassa asingeingia Chadema, Ukawa hii ya leo ingeishia njiani.”

PILI

“Jambo la pili ni kupungua nguvu kwa Chadema. Kwa miaka yote nyuma, Chadema kimekuwa kikizidi kuimarika kila baada ya uchaguzi, lakini mwaka huu kitapungua nguvu.“Kitapungua nguvu kwa sababu, wana mpasuko wa chini kwa chini lakini unazibwa na harakati za umoja kuelekea uchaguzi mkuu wakiamini watachukua dola mwezi ujao. Kama nilivyosema Ukawa itasambaratika. Hiyo itachangia kupungua nguvu kwa Chadema.”

TATU

“Lakini kuna jambo lingine la tatu. Lowassa ni mwanasiasa kwa sasa lakini ili aendelee kuwa mwanasiasa ni lazima apate ushindi mwezi ujao. Akishindwa, itabidi aachane na siasa kwa sababu, kwanza umri utakuwa umekwenda.
“Kwa sasa ana miaka 62, kuja kugombea tena ni miaka mitano mbele ambapo atakuwa na miaka 67. Atakuwa amechoka na hatakuwa na nafasi yoyote ndani ya chama. Pia, kwa misukosuko hii ya kampeni, atakuwa amechoka sana na atakabiliwa na mavune (uchovu baada ya shughuli nzito).”

NNE

“Nimekuwa nikikiangalia kwa umakini sana Chama Cha ACT-Wazalendo. Ni chama chenye sera nzuri kwa sababu kinasimamia kupiga vita ufisadi. Endapo Lowassa atashindwa kwenye uchaguzi ujao, kama nilivyosema awali, Chadema kitapungua nguvu, hivyo ACT ndiyo chama kinachokuja kuwa kikubwa cha upinzani hapa Tanzania.”

TANO

“Lakini pia kama Lowassa ataanguka, ina maana CCM itarudi madarakani kwa sababu ndiyo chama tawala chenye nguvu katika kinyang’anyiro hiki kikifuatiwa na Chadema.“Katika historia ya uchaguzi hapa Tanzania, hakuna mwaka ambao CCM imewahi kupata wakati mgumu kama mwaka huu wa 2015. Nimewahi kuzungumza na kiongozi mmoja wa CCM wa ngazi ya juu, aliniambia hata wao hawalali usingizi mwaka huu.

“Hii inatokana na ukweli kwamba, Lowassa kuhamia Chadema kumezidisha ushindani. Kwa hiyo, kama Lowassa ataanguka, CCM kitajiimarisha zaidi kuliko mwaka mwingine wowote. Hakitakubali kusimamia uzembe, kuangalia makosa wala kulegea kwenye utekelezaji wa ilani zake.”

MWENENDO WA SIASA

Kuhusu mwenendo wa kisiasa nchini, mchambuzi huyo alisema anasikitishwa na tabia za baadhi ya vyama kutengenezeana skendo ili upande wa pili uonekane hovyo.

“Kuna watu walisema wamenasa ‘chating’ ya Mwigulu Nchemba, Januari Makamba, Livingstone Lusinde (Kibajaj) na Angella Kairuki kwenye Mtandao wa WhatsApp eti wakizungumzia mikakati ya kujipanga upya katika kampeni kwa madai kwamba wanazidiwa na Lowassa.

“Hivi kwa akili za kawaida, Makamba ni naibu waziri wa mawasiliano na teknolojia, anaweza kutumia mtandao kuzungumzia mambo hayo kweli? Tena kwa kuchati badala ya kupiga?!
“Yale ni mambo ya kisiasa. Upande mmoja kutengeneza skendo ili kuuumiza upande mwingine. Ni hatari. Naviasa vyama vyote kuachana na siasa hizi za maji taka.”

JIUNGE NA GLOBAL BREAKING NEWS!

Leave A Reply