Askari wa bunge wakibeba jeneza la mwili wa Dk. Abdallah Kigoda.
Jeneza lenye mwili wa marehemu Dk. Kigoda.
Wanafamilia wa marehemu Dk. Kidoga wakionesha nyuso za huzuni.
Kutoka kulia ni Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilal, akifuatiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na rais mstaafu wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi wakiwa kwenye maombolezo hayo.
Aliyekuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anne Makinda, akizungumza jambo kwenye maombolezo hayo.
Viongozi wakuu wa kiserikali wakijiandaa kutoa heshima za mwisho.
Bilal akitoa heshima mbele ya jeneza la mwili wa Dk. Kigoda.
Mizengo Pinda akitoa heshima za mwisho.
Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamini Mkapa, akitoa heshima za mwisho.
MAKAMU wa Rais, Dk.Gharib Bilal, Waziri Mkuu, Mizengo Kayanza Pinda, wameongoza kuuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda, aliyefariki Oktoba 12 mwaka huu wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Apollo nchini India.
Akitoa pole za rambirambi kwa wafiwa, Spika wa Bunge la Tanzania aliyemaliza muda wake, Anne Makinda, amesema kuwa msiba huo ni pigo la nne mfululizo kwa Bunge la Tanzania tangu kuvunjwa kwake.
Makinda akizungumza leo wakati wa kuuaga mwili wa Kigoda kitaifa katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam, amesema bunge limepata msiba mkubwa mwingine tangu kuvunjwa kwake ambapo katika uongozi wake limepoteza wabunge 12.
Makinda amesema Dk. Abdallah Kigoda alikuwa ni mtumishi aliyetukuka na hodari aliyeweza kupanua wigo kwa wawekezaji na wafanyabiashara kiasi cha kukuza uchumi wa taifa kwa kutoa ajira na kuchochoea maendeleo ya taifa.
Mwili wa marehemu Kigoda umesafirishwa kwenda nyumbani kwake Handeni mkoani Tanga kwa ajili ya maziko yanayotarajiwa kufanyika jioni leo huku ikitarajiwa mazishi hayo yataongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.
Kifo cha Kigoda ambaye alikuwa mgombea wa ubunge Jimbo la Handeni Mjini, kimesababisha kampeni za ubunge mjini hapo kuahirishwa ili kusubiri ratiba mpya ambapo Chama Cha Mapinduzi (CCM) kitaruhusiwa kuteua mgombea mwingine.
Mgombea huyo ni wa nne kufariki ambapo wengine ni Mohamed Mtoi wa Chadema aliyekuwa akigombea Jimbo la Lushoto, mwingine ni Celina Kombani wa CCM aliyekuwa akigombea Jimbo la Ulanga na Estomi Malla wa ACT-Wazalendo wa Arusha Mjini.
(NA DENIS MTIMA/GPL)