The House of Favourite Newspapers

Mabilionea Wasio na Huruma 60

0

nigerianfm-500-dollars1Dk. Viola na Vanessa, mabilionea wanawake wawili hatari ambao waliapa tangu wakiwa watoto wadogo kwamba kwao kutajirika lilikuwa ni jambo la lazima, wakatumia elimu walizozipata, Dk. Viola akiwa bingwa wa magonjwa ya figo ambaye alitumia elimu hiyo kuwaibia watu figo zao na kuziuza kwa wagonjwa wa figo matajiri duniani ambako alilipwa mpaka dola milioni moja kwa figo moja.

Vanessa akiwa mhandisi wa ndege akifanya kazi kwenye Shirika la Ndege la Brito Africa Airline la Uingereza, alishirikiana na Dk. Viola kuangusha ndege iliyoua abiria wote zaidi ya mia mbili, kati yao wakiwemo yatima 62 waliokuwa wakisafiri kutoka Tanzania kuelekea Uingereza mwenyeji wao akiwa Vanessa.

Yatima hao 62, wiki mbili kabla ya ajali hiyo kutokea, Dk. Viola aliwawekea bima ya maisha na kujitaja yeye mrithi wa fidia zao ikitokea wakafa, kitendo hiki kilimfanya ajipatie dola milioni 620, kwani kila mtu aliyekufa katika ajali hiyo alilipwa fidia ya dola milioni kumi! Fidia hiyo pamoja na fedha ambazo Dk. Viola alikuwa nazo, zilimfanya afikie utajiri wa dola bilioni moja akiwa na umri mdogo.

Baada ya tukio hilo la kuanguka kwa ndege, Vanessa aliacha kazi mara moja na kuondoka nchini Uingereza kurejea Tanzania ambako aliungana na ndugu yake kuendesha shughuli zao za kibiashara, haukupita muda mrefu sana wakauza kila kitu ikiwa ni pamoja na kubomoa nyumba ambayo Dk. Viola alikuwa akiishi na kusafiri kwenda Thailand ambako daktari bingwa wa upasuaji wa plastiki, Jeremy Ho aliwabadili sura zao na kuwafanya waonekane kama wazee wa Kijapan.

Wakarejea Tanzania kama wawekezaji na kununua Kisiwa cha Bongoyo ambako walijenga mji wa kisasa wakiheshimiwa na kila mtu nchini Tanzania, hakuwepo mtu wa kuwagusa! Mpelelezi mmoja aitwaye Inspekta Masala ndiye aliyekuja nchini humo na kutibua kila kitu, wakakamatwa na kufikishwa mahakamani ambako hivi sasa kesi ya mauaji inaendelea.Je, nini kinaendelea kwenye kesi hii? SONGA NAYO…

MIFUPA iliyoingizwa ilikuwa haitoi harufu yoyote, ilikauka vizuri! Ilikuwa mingi mno iliwachukua askari waliokuwa wakisomba muda wa kama dakika kumi, jaji akaamuru zoezi hilo lisimamishwe baada ya vifaa vya upasuaji vilivyotolewa chini ya ardhi mahali palipokuwepo nyumba ya Dk. Viola.

“Inatosha!” Jaji aliongea.
“Mheshimiwa Jaji haya ni mabaki ya mifupa iliyochimbuliwa chini ya bustani ya jiji ambayo inajulikana kwa jina la City Park, iliyotolewa na Dk. Viola kwa jiji baada ya kubomoa jumba lake la kifahari, alifanya hivyo kuficha siri ya makaburi ya watu aliowaua yaliyokuwepo chini ya ardhi ambao aliwazika baada ya kuwaibia figo zao, naomba kuwakilisha.”

Dk. Viola alikuwa kimya, ghafla machozi yakaanza kumtoka, baada ya kuishuhudia mifupa hiyo, alionekana kama mtu aliyeingiwa na majuto moyoni mwake.

Watu walipomwangalia walimwona kama mtu aliyekuwa anaigiza ili aonewe huruma kwani unyama alioufanya haukuwahi kufanywa na mwanamke mwingine yeyote chini ya jua.
“Kama huna swali jingine basi anaweza kuondolewa mahakamani ili uendelee na mshtakiwa wa pili,” Jaji alimalizia na watu wakashuhudia Dk. Viola akiondolewa kizimbani na baadaye kupelekwa nje kabisa ya ukumbi wa mahakama akiwa chini ya ulinzi.

Ukumbi wa mahakama ulikuwa kimya, ndugu wa marehemu wakiendelea kububujikwa na machozi, mioyo yao ilikuwa imeumia, walitamani angalau waelewe mifupa hiyo ilikuwa ni ya nani na nani lakini haikuwezekana, ilikuwa ni mingi mno kutambua mifupa ya ndugu zao.

Kwikwi ziliendelea kusikika bila watu kutoa sauti, picha mahakamani hapo ilifanana kabisa na siku ya msiba, ukimya uliongezeka, mwanamke mwingine aliyefanana na sura ya mwanaume wa Kijapan aliposimamishwa kizimbani.
“Unaweza kumuuliza maswali sasa mshtakiwa wa pili,” Jaji aliongea.
“Ahsante mheshimiwa Jaji.”

Mwanasheria wa Serikali, Anganile Hosea, alikisogelea kizimba cha Vanessa na kukigusa, akamwangalia kwa karibu dakika mbili bila kusema kitu chochote, Vanessa pia alikuwa akimkodelea macho huku uso wake ukiwa umefunikwa na tabasamu.
“Jina lako?”

“Naitwa Vanessa Benedict Kabyenge”
“Taaluma yako?”
“Mhandisi wa ndege.”
“Jinsia?”
“Mwanamke.”
“Wewe ni mwanamke?”
“Ndiyo.”

“Mbona unaonekana kama mzee wa Kijapan?”
“Nilibadili sura.”
“Sababu?”
“Sikutaka kuolewa, hivyo nikataka nifanane na mzee wa Kijapan.”
“Ohoo! Umewahi kufanya kazi Shirika la Ndege la Brito Africa Airline?”
“Ndiyo.”

“Unakumbuka ajali ya ndege iliyoua watu zaidi ya mia mbili?”
“Ndiyo.”
“Nani alihudumia ndege hiyo kabla haijaruka?”
Vanessa alikaa kimya kwa karibu dakika tatu akitafakari, jasho likimtoka ingawa hali ya hewa katika Jiji la Dar es Salaam wakati huo ilikuwa ya ubaridi, lilikuwa swali rahisi lakini gumu sana kwake kwani lilielekea kwenye kumweka kikaangoni ambako angeshindwa kujinasua kama angejibu vibaya.

“Nimekuuliza nani alihudumia ndege hiyo ambayo baadaye ilikwenda kuanguka?”
“Mimi.”
“Uliihudumia vizuri?”
“Ndiyo.”
“Mtu wa mwisho kuhudumia injini yake alikuwa nani?”
“Kijana aitwaye Davis.”

“Una uhakika?”
“Asilimia mia moja.”
Mwanasheria Anganile akakiacha kizimba na kumwangalia Jaji aliyekuwa kimya akisikiliza, akapiga hatua tatu mbele mpaka karibu kabisa na meza ya Jaji kisha kusogeza meza nyingine iliyokuwa kando, juu yake kukiwa na projekta, akaiwasha na kumulika pembeni kwenye kitambaa cheupe, picha zikaanza kuonekana za Ndege ya Shirika la Ndege la Brito Africa Airline, iliyokuwa ikifanyiwa matengenezo kabla ya kuruka.

Vanessa akaonekana akiwa amevalia ‘ovaroli’ ya rangi ya khaki iliyokuwa imejaa uchafu mwingi wa oil, alikuwa akiwasimamia vijana zaidi ya kumi kuifanya kazi hiyo.
“Kati ya hao vijana wanaoonekana, Davis ni yupi?”
“Aliyevalia ‘ovaroli’ ya rangi ya kijani.”
“Ndiye alikuwa wa mwisho kuihudumia injini ya ndege?”
“Ndiyo.”

Mwanasheria Anganile akanyanyua kichwa chake na kumwangalia Jaji na kumwomba atulie ili wote waangalie mtu wa mwisho kuhudumia injini ya ndege alikuwa nani, sinema ikaanza kutembea mahakamani, mwisho kabisa kazi ilipomalizika vijana wote pamoja na Vanessa waliondoka lakini yeye Vanessa akarejea dakika kumi baadaye akiwa ameshikilia kiboksi kidogo, Mwanasheria Anganile akakivuta kiboksi hicho kukikuza ili maandishi juu yake yasomeke vizuri halafu akakigandisha.

“Naomba uisomee mahakama tukufu hayo maandishi yameandikwaje?”
“Yameandikwa Xplo-Corrosive!”
“Ni kitu gani hicho?”
“Milipuko.”

“Ulikuwa unaipeleka kwenye injini ya ndege kwa ajili ya kazi gani?”
Vanessa hakuweza kujibu swali hilo, akageuka bubu! Mwanasheria akamwamba Jaji aupokee mkanda huo wa video kama ushahidi kwenye kesi hiyo ya mauaji, lengo lake lilikuwa ni kuiaminisha mahakama kwamba Vanessa alitega milipuko ndani ya ndege hiyo ili iue watu waliokuwa ndani yake.

“Nikisema ulitega milipuko ndani ya ndege hiyo ili ianguke na kuua abiria wote ikiruka kutoka Tanzania kurejea Uingereza wakiwemo yatima 62 ndani yake mliokuwa mmetengeneza mpango wa kuwaua ili wewe na pacha yako Dk. Viola mlipwe dola milioni 620, utasemaje?”
“Ni uongo.”

“Kwa nini uliacha kazi muda mfupi tu baada ya ajali hiyo?”
“Kwa sababu nilikuwa nimechoka kuishi Uingereza na nilitaka kurejea nyumbani Tanzania.”
“Kwa hiyo huhusiki kabisa na dola milioni 620?”
“Sihusiki nazo.”

Mwanasheria Anganile akatembea hadi kwenye meza yake na kuchukua bahasha, ndani yake akatoa karatasi nyeupe na kurejea tena hadi kwenye kizimba cha Vanessa akamwonyesha barua hiyo akimtaka asome kilichokuwa kimeandikwa juu yake.
“Soma!”
“Wezesha Mzawa Commercial Bank!”
“Endelea.”

“Account Holders” (Wenye Akaunti!)
“Wataje.”
“Dr. Viola Benedict Kabyenge and Vanessa Benedict Kabyenge!”
“Endelea.”

“Balance 620 million USD!”(Salio ni dola milioni 620)
“Endelea.”
“Paid by Britain Insurance” (Imelipwa na Britain Insurance)
“Bado unakataa kwamba huhusiki na fedha za fidia?”
Vanessa kwa mara nyingine tena hakuwa na jibu.

Je, nini kitaendelea? Fuatilia kesho katika Gazeti la Championi Jumamosi.

Leave A Reply