Kampuni ya Simu za mkononi ya Airtel Tanzania kupitia kampeni yao ya “Airtel Tunakujali” inayoendeshwa na wafanyakazi wake imekabidhi darasa kwa shule ya msingi kumbukumbu Jijini Dar es Salaam ambalo imelikarabati kwa ajili ya wanafunzi wa awali maarufu kama chekechea.
Mkurugenzi Mkuu wa Airtel Tanzania Sunil Colaso alielezea umuhimu wa ukarabati wa darasa la chekechea kwa wafanyakazi wa Airtel.
Leo Airtel, kupitia mpango wetu wa “Airtel Tunakujali”, tunatimiza dhamira yetu tuliyotoa ya kuwezesha shule ya msingi Kumbukumbu kuwa na uhakika na mazingira salama ya kusomea kwa wanafunzi wawapo hapa shuleni.
Kwani elimu bora huanzia kwenye hatua ya awali hivyo ukarabati wa darasa hili utakuza chachu ya wanafunzi hawa wadogo kujijengea mazingira ya kupenda kusoma wakiwa wakubwa”.
Akifafanua amesema, “wanafunzi wanapokuwa shuleni walimu huwa watu muhimu sana kwao, kwani huwafundisha watoto misingi bora ya kuishi hapa duniani, ambapo uwepo wa mazingira mazuri ya kufundishia huwapa morali walimu.
Ushirikiano wetu na shule ya msingi Kumbukumbu hautaishia hapa kwani tumepanga kuiwezesha ili iwe shule bora ndani ya manispaa ya Kinondoni na taifa kwa ujumla” aliongeza.
Akishukuru kwa niaba ya wanafunzi wenzake mtoto Clara Joshua amesema , “sasa watasoma katika darasa lenye hewa safi kwani ni kubwa sana na pia wataweza kujifunza vizuri zaidi”.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kumbukumbu Pricilla Moshi akitoa shukurani zake kwa Airtel amesema, “tunawashukuru sana Airtel kwa kuweza kukarabati darasa la watoto wetu wa chekechea kwani halikuwa katika mazingira mazuri. Sasa hivi lina hewa ya kutosha na mtazamo mzuri kabisa. Napenda kutoa shukurani zangu kwa dhati kwa msaada huu.”
Kupitia Airtel Tunakujali, tayari shule za msingi na sekondari zimenufaika kwa kujengewa, kukarabatiwa na kukabidhiwa vitabu kutokana na fedha zinazochangwa na wafanyakazi wa kampuni hiyo tokea uanze hapo mwaka jana, na huu ni mwanzo kwani bado shule nyingine nyingi zitaendelewa kufikiwa.