The House of Favourite Newspapers

ALAT: Vyanzo vya Mapato vya Halmashauri Virudishwe

0
Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, akizungumza katika ufunguzi wa mkutano wa Jumuiya ya Tawala na Serikali za Mitaa (ALAT) leo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wajumbe waliohudhuria mkutano huo.
Mmoja wa wajumbe wa mkutano huo akichangia jambo.

 

MWENYEJI wa mkutano wa 33 wa Jumuiya ya Tawala na Serikali za Mitaa (ALAT) ambaye ni  Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, amesema kupitia mkutano huo wataiomba serikali  irudishe vyanzo vya mapato vilivyokuwa katika halmashauri.

 

Meya Mwita alisema hivyo leo wakati akitoa salamu za kuwakaribisha wajumbe wa mkutano wa ALAT unaofanyika jijini Dar es Salaam.

 

Mwita alisema vyanzo vya mapato ambavyo vilikuwa vikisimamiwa na halmashauri na majiji viliwezesha kuleta maendeleo katika nyanja mbalimbali hususani huduma za kijamii.

 

Alifafanua kuwa vyanzo hivyo kuwa ni matangazo ya barabarani sambamba na kodi za majego ambavyo kwa kiasi kikubwa vilikuwa vikiziletea halmashauri fedha ambazo zilitumika kuboresha huduma za afya, elimu na barabara.

 

Aliongeza kuwa kwa kuzingatia ustawi wa halmashauri hizo, mkutano huo utajadili suala hilo na kumfikishia Rais John Magufuli ili fedha hizo zirudi kwa ajili ya maendeleo hususani vijijini, kata na majiji.

“Hali ya halmashauri nyingi kifedha si nzuri, na hii ni baada ya vyanzo hivi vya mapato ambavyo tulikuwa tunavitegemea kuchukuliwa. Katika hali hii hakuna halmashauri ambayo itakuwa na fedha, ” alisema.

 

Alitolea mfano halmashauri ya Ilala katika jiji la Dar es Salaam ambayo kupitia vyanzo hivyo ilikuwa ikikusanya zaidi ya Sh. bilioni 68 ambazo zilikuwa msaada mkubwa katika kutoa huduma za kijamii ndani ya halmashauri hiyo.

 

Mbali na changamoto za mapato ambazo halmashauri zinakabiliana nazo, alisema changamoto nyingine ni kuhusu hali za madiwani hususani kifedha kuwa imekuwa ngumu.

 

“Hali ya madiwani kifedha imekuwa ngumu katika utendaji wao  wa kila siku kwa sababu wanalipwa shilingi 350,000 kwa mwezi ambazo hazitoshi kutokana na gharama za usafiri anazotumia kuzungukia maeneo yao,” alisisitiza.
Baadhi ya vyanzo vya mapato vilivyokuwa kwenye halmashauri mbalimbali vilihamishiwa serikali kuu.

 

Leave A Reply