The House of Favourite Newspapers

Amuua mkewe kwa kumpiga na mti

0

TARIME KIFONa Igenga Mtatiro, UWAZI

MARA: Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Tarime na Rorya mkoani hapa, linamshikilia Hamis Nyamasinda, mkazi wa Kitongoji cha Ramboni, Kijiji cha Nyangoto, Nyamongo wilayani Tarime kwa tuhuma za kumuua mkewe, Bhoke Hamis Nyamasinda kwa kumpiga na mti sehemu mbalimbali za mwili wake.

Kwa mujibu wa taarifa za jeshi la polisi, mtuhumiwa huyo alitenda unyama huo Juni 30, mwaka huu kijijini hapo, kufuatia migogoro ya mara kwa mara ya wanandoa hao, mwanaume akimtuhumu mkewe kwamba hakuwa akiiheshimu ndoa yao.

Kwa mujibu wa majirani wa wanandoa hao, siku ya tukio, kulitokea ugomvi kati yao kabla ya mwanaume huyo kuanza kumshambulia mkewe sehemu mbalimbali za mwili wake kwa mti na kumsababishia maumivu makali na baadaye kupoteza fahamu.

“Alimuumiza sana kwa kweli, tukisaidiana na baba yake, mzee Alphaxade Bukimba, tulimpeleka Kituo cha Afya cha Nyangoto akiwa hajitambui, baadaye alifariki dunia,” alisema shuhuda mmoja aliyeomba hifadhi ya jina lake na kuongeza:

“Mara kwa mara walikuwa wakipigana, mume alikuwa akimtuhumu marehemu kwamba haheshimu ndoa yao.”

Marehemu ameacha watoto watatu, Jackline, Roby na Lulu ambao wote bado wana umri mdogo, wa kwanza akiwa anasoma darasa la pili katika Shule ya Msingi Nyamongo, wa pili akiwa anasoma darasa la kwanza na wa mwisho akiwa bado hajaanza shule.

Ofisa mmoja wa polisi wilayani Tarime amethibitisha kukamatwa kwa Hamisi lakini hakuwa tayari kuelezea zaidi kwa kuwa siyo msemaji.

Leave A Reply