The House of Favourite Newspapers

Anaswa Akimiliki Kiwanda cha Kutegenezea Silaha za Moto

0

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linamshikilia, Shabani Athumani (61) mkazi wa Kwamakocho, Chalinze akituhumiwa kumiliki kiwanda cha kutengenezea Silaha mbalimbali za moto.

 

 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Wankyo Nyigesa, amewaambia waandishi wa habari jana kuwa tukio la kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo limetokea Januari 31, saa 1 jioni.

 

 

Kwa mujibu wa Nyigesa, kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kulitokana na ushirikiano wa raia mwema na kwamba baada ya kupata taarifa hizo walifanya uchunguzi na kisha kubaini uwepo wa kiwanda hicho.

 

 

Amesema katika uchunguzi huo Jeshi la Polisi lilimkamata mtuhumiwa huyo akiwa na mtambo wa kufulia vyuma, chupa 5 ndogo zenye baruti ndani yake, Fataki 48 na risasi 42 za bunduki aina Gobole na Paketi 1 ya unga wa Kiberiti.

 

 

Wankyo ametaja vifaa vingine kuwa ni mitambo mitatu ya Silaha aina ya Gobole ambayo ipo tayari bado kuwekwa mtutu na kitako, mitambo ya kutobolea vifaa vya miti vinavyotumika kwenye silaha aina Gobole na kopo moja lenye unga wa tindikali ambalo unatumika kuunganisha vyuma vinavyofungwa kwenye silaha aina ya gobole.

 

 

“Mtuhumiwa tumemkamata akiwa anamiliki kiwanda cha kutengenezea Silaha na vifaa vya silaha za kienyeji na kwamba uchunguzi bado unaendelea na baadae kufikishwa Mahakamani.

 

 

“Atafikishwa mahakamani mara moja kwa ajili ya kujibu tuhuma zake niwaobe wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi,” amesema.

 

 

Aidha, katika tukio lingine Jeshi hilo limefanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja ambaye jina lake limehifadhiwa akiwa anamiliki bunduki tatu aina ya short gun na gobole moja,risasi 13 za shortgun na maganda matatu ya risasi.

 

 

Kamanda Nyigesa amesema mtuhumiwa huyo alikamatwa Januari 21, mwaka huu saa 6:30 usiku katika maeneo ya Pingo Wilaya ya Kipolisi Chalinze Mkoa wa Pwani.

 

 

Amesema mbali na vifaa hivyo lakini vingine ni Cocking handle mbili, goroli 60, misumeno miwili ya kukatia mbao na chuma, plaizi moja, bisibisi moja, kipande cha mtutu wa bunduki, vipande vidogo vya chuma sita, vipande vya miti vyenye chuma ndani vinne na mitambo ya kutengenezea bunduki miwili.

 

 

Hata hivyo, Nyigesa amesema watuhumiwa wengine waliohusika katika tukio hilo bado Jeshi la Polisi linaendelea kuwasaka na wakikamatwa watachukuliwa hatua ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

 

Leave A Reply