Auawa kwa hawara, kaburi lazikwa kichwa cha kondoo!
Nyangi Masengi Nyangi enzi za uhai wake.
Na Gregory Nyankaira, UWAZI
MARA: Mkazi mmoja wa kitongoji cha Jiniva, Kijiji cha Kiabakari, Kata ya Kukirango, Wilaya ya Butiama mkoani Mara, Nyangi Masengi Nyangi (37), ameuawa kikatili kwa kukatwakatwa na mapanga na watu wasiojulikana, akiwa nyumbani kwa hawara yake.
Mke wa marehemu akiwa amejeruhiwa kwenye paji la uso.
Watu walioshuhudia tukio hilo lililotokea usiku wa Juni 22, mwaka huu, majira ya saa mbili, katika Kijiji cha Mwikoro, walisema Nyangi anayemiliki ng’ombe 80 nyumbani kwake katika Kitongoji cha Jiniva, anadaiwa kuiba ng’ombe Juni 21, mwaka huu saa 7.00 usiku katika Kijiji cha Kamugegi na kumpeleka kwa hawara yake huyo kwa nia ya kwenda kumuuza mnadani siku inayofuata huko Kiabakari.
Walidai kuwa baada ya Nyangi kumficha ng’ombe huyo, alimuita mke mkubwa anayeishi Kijiji cha Kitenga,Tarime ambaye alikwenda na kuungana na mumewe.
Kondoo akichinjwa.
“Wakiwa wanakula chakula cha usiku kwa hawara yake saa 2.00 usiku, Nyangi, mkewe mkubwa na watoto wa hawara yake huyo, ghafla walijikuta wanavamiwa na kundi la watu wakiwa na mapanga, marungu na pinde,” alisema mmoja wa mashuhuda na kuongeza kuwa baada ya kukamatwa na watu hao, Nyangi na mkewe walianza kupigwa huku wakimtaka mwanaume huyo kuonesha alipo ng’ombe wao, jambo lililofanya awaoneshe kabla ya kumzidishia kipigo kilichomuua.
Kichwa cha kondoo kikizikwa kaburini.
Katika hatua nyingine, mazishi ya marehemu Nyangi yalileta utata wa sehemu ya kufanyika baada ya makaburi mawili kuchimbwa, kwa mke mdogo na mkubwa wanaoishi katika vijiji viwili tofauti.
Jeneza lenye mwili wa marehemu.
Awali mama mzazi wa marehemu alitaka mwanaye azikwe kwa mkewe mdogo katika Kijiji cha Jiniva, lakini wakati kaburi likiwa limeshachimbwa, wanandugu wengine waliibuka na kupinga wakitaka akazikwe kwa mkewe mkubwa, huko kwenye Kijiji cha Kitenga jambo ambalo hatimaye lilikubalika.
Waombolezaji wakiwa msibani.
Lakini kabla ya kuondoka kuelekea huko, kwa mujibu wa desturi, wanandugu walilazimika kumchinja kondoo na kuzika kichwa chake katika kaburi lililochimbwa ndipo waliposafirisha mwili kwa mazishi yaliyofanyika Juni 25, mwaka huu.
Kaburi kilimozikwa kichwa chakondoo.
Polisi wilayani Butiama imethibitisha kuwepo kwa tukio hilo na wanaendelea na uchunguzi huku ikiwaonya wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi.