The House of Favourite Newspapers

Aucho, Diarra Warudishwa Fasta Yanga

0

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mtunisia, Nasreddine Nabi, amecharuka kwa kuwataka wachezaji waliokuwepo katika majukumu ya timu zao za timu za taifa akiwemo kiungo mkabaji, Mganda, Khalid Aucho na kipa Djigui Diara wote mwisho kuripoti kambini.

 

Hiyo ni katika kuelekea mchezo wa hatua ya awali wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Rivers United ya nchini Nigeria utakaopigwa Jumapili hii kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.Wachezaji waliokuwepo katika majukumu ya timu ya taifa, nchi zao zinawania kufuzu kucheza Kombe la Dunia litakalofanyika mwakani nchini Qatar.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Spoti Xtra, kutoka ndani ya benchi la ufundi la timu hiyo, kocha huyo juzi Jumapili jioni aliwataka mabosi wake kuhakikisha wanafanikisha tiketi za nyota hao ili wafike kwa muda alioupanga wa wachezaji wote kuripoti kambini jana Jumanne saa moja usiku.

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa Aucho na Diarra tayari wametumiwa tiketi ya ndege ambayo hadi kufikia jana saa moja usiku wanatakiwa kuripoti kwa ajili ya kuanza maandalizi ya pamoja ya mchezo huo dhidi Rivers.

 

Alisema kuwa pia wachezaji waliokuwepo katika kikosi cha Taifa Stars akiwemo Bakari Mwamnyeto, Dickson Job na Feisal Salum ‘Fei Toto’ wametakiwa kuripoti kwenye kambi ya timu hiyo Avic Town, Kigamboni, Dar baada ya mchezo wao dhidi ya Madagascar.

 

“Kocha Nabi hataki masihara katika kuelekea mchezo wetu dhidi ya Rivers kwani haraka amewataka wachezaji wote waliokuwepo katika majukumu ya timu za taifa kuripoti kambini muda alioupanga.

 


“Kwa wale wachezaji waliokuwepo
katika majukumu ya timu za taifa hasa wale wa nje ya Tanzania wakiwemo Aucho na Diarra nao wametakiwa kuripoti muda huo ndiyo utakuwa mwisho kwani wao majukumu yao yamemalizika jana (juzi Jumatatu).

 

“Tayari tumewatumia tiketi zitakazowafanya wafike kwa muda huo uliopangwa na kocha, kwa wale waliokuwepo Taifa Stars nao watatakiwa kuripoti kambini katika muda huohuo baada ya mchezo dhidi ya Madagascar,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Akizungumzia hilo, Meneja Mkuu wa Yanga, Hafidh Saleh, alithibitisha kwa kusema: “Wachezaji wetu wote waliokuwepo katika majukumu ya timu za taifa watatakiwa kuripoti kwa wakati kambini kesho (jana Jumanne) tayari kwa ajili ya kuanza maandalizi ya mchezo huo wa kimataifa.”

Leave A Reply