The House of Favourite Newspapers

BAADA YA KUPATANA… DIAMONDI BABA’KE WAFUKUA MAKABURI

DAR ES SALAAM: WIMBO mpya wa Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ wa The One umeshindwa kuzima kishindo cha tukio la msanii huyo kupatana na baba yake mzazi, mzee Abdul Juma; Ijumaa linakupakulia uhondo kamili. 

 

Kama ulivyosikia siku chache zilizopita kwamba baba na mwanaye wamemaliza bifu lao lililodumu kwa miongo kadhaa, jambo ambalo kusema kweli limefukua makaburi.

MAMBO YALIYOFUKULIWA

Mambo yaliyofukuliwa siku msanii huyo na baba yake walipofanyiwa mahojiano maalum na redio moja hapa nchini ni yale ambayo yamewahi kuripotiwa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii na kuonekana kama yamepita.

 

Mfano; uhusiano wa kimapenzi kati ya Diamond na Wema Isaac Sepetu, Hamisa Mobeto, Irene Louis ‘Lynn’, kutengana kwake na Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ na kutotunza watoto aliozaa na Zari, Princess Tiffah na Prince Nillan. Mengine ni ‘mtungo’ wa Diamond kwa wanawake, kununua nyumba Afrika Kusini, uhusiano wake mpya na Tanasha Donna pamoja na bifu lake na baadhi ya wasanii wenzake na mambo mengineyo kibao.

TUDADAVUE KIDOGO

Tukio kubwa katika mahojiano hayo maalum lilikuwa ni la Diamond kumaliza bifu lake na baba yake ambapo mjadala mkubwa ulikuwa ‘kwa nini iwe sasa?’

Wachangiaji wengi wenye mitandao walisema huenda mapatano hayo yamefanywa na msanii huyo kubusti wimbo wake ambao unadaiwa kuwa umeshindwa kukiki kwa viwago vilivyozoeleka na mashabiki. “Watu wamepiga kelele, wameandika habari na makala nyingi kumsihi Diamond amtunze baba yake, lakini hakufanya hivyo, leo kaona hana pa kupatia kiki ndiyo kaamua kurudi kwa mzee wake,” mchangiaji mmoja aliweka komenti yake kwenye moja ya posti iliyowekwa Mtandao wa YouTube.

MAJIBU YA DIAMOND KATIKA HILI

Hata hivyo, Diamond katika mahojiano yake na redio hiyo alisema, hajawahi kuwa na bifu na baba yake na kwamba vyombo vya habari vilikuwa vinakuza ugomvi kati yao. Kuhusu wimbo wake ‘kupooza’ msanii huyo alisema hilo limetokana na mashabiki wake kuhisi angetoa wimbo wenye midundo na staili ya vijanavijana, alipotoka kivingine watu wanaona kama umeshindwa kukiki.

 

BABA DIAMOND KANUNULIWA

Mara baada ya kufanyika mapatano hayo, habari zilienea na madai kuwa mzee Abdul alishikishwa hela ndefu na mameneja wa Diamond ili akubali kupatanishwa na mwanaye lengo likiwa ni lilelile la kutengeneza kiki.

Gazeti la Ijumaa lilipomtafuta mzee Abdul ili ajibu madai hayo ambapo alisema kwa kifupi; “Hakuna kitu kama hicho, kwanza mimi sikutegemea kama hilo lingefanyika, nimefurahi sana kuweka mambo sawa na mwanangu, nayaona mambo mema mbele yangu na kwa mwanagu,” alisema mzee Abdul.

 

KUHUSU NYUMBA

Kaburi jingine lililofukuliwa ni ishu ya Diamond kununua nyumba nchini Afrika Kusini ambayo zamani iliripotiwa na kuzua gumzo kisha kupoa, lakini juzi mjadala uliibuka upya kwa baadhi ya watu kusema msanii huyo hana jeuri hiyo. “Yaani anunue nyumba Afrika Kusini halafu amwanchie mwanamke kirahisi tu! “Kama nyumba ingekuwa yake mbona alipotaka kwenda na wasanii wa Bongo kwenye sherehe ya kuzaliwa mwanaye Tiffah, Zari alisema hataki wakanyage huko kwa sababu watamchafulia nyumba yake?

“Labda aseme kuwa alichagia senti kidogo wakanunua; yaani nyumba yake halafu Zari aingize mwanaume mwingine na kuposti picha mitandaoni wakiwa ndani, duh!” Mchangiaji mwingine kwenye Mtandao wa YouTube aliandika komenti hii. Hata hivyo, wakati Diamond anahojiwa alisema kwamba nyumba hiyo ni yake na kwamba hati na nyaraka zote anazo na anao uwezo wa kuiuza wakati wowote, lakini ameacha wanaye waishi.

 

MTUGO NAO WAZUA JAMBO

Katika mahojiano hayo msanii huyo alisema kuwa ni kweli amekuwa akideti na wanawake wengi kwa siku za nyuma, lakini sasa ameamua kutulia kwa sababu amempata mpenzi anayejitambua; Tanasha. Kauli hiyo nayo iliibuka kwa upya mitandaoni baada ya baadhi ya watu kuposti video na sauti za Diamod zilitoa maneno kama hayo wakati alipoanza uhusiano na Zari. “Haamini huyo jamaa, alipokuwa na Wema alisema kafika; akachepuka. Akampata Zari akasema, ametulia, hakutulia chochote zaidi ya kuzidi kurukaruka kwa wanawake, aibu kwa wanaojirahisi kwake,” mwingine aliandika.

TANASHA ASIFIWA

Kuthibitisha kwamba chagua la sasa kalifanya kwa umakini mkubwa, Diamond alimwagia sifa mpenzi wake, Tanasha kuwa ni mtu mwelewa na kwamba yeye si mtu wa mitandao ya kijamii kama walivyokuwa wanawake zake wengine. Hata hiyo, wenye maneno yao waliponda kauli hiyo kwa kusema msichana huyo kutoka Kenya hana mvuto na kwamba anaizima nyota yake na kukumbushiwa enzi za uhusiano wake na Wema na Zari ambapo alionekana kuwa juu kisanii kuliko alivyo hivi sasa.

 

ZARI AANZISHA VITA

Kuonesha kwamba siku hiyo ya upatanisho ilikuwa na mengi mazito, Diamond alifungukia uhusiano wake na Zari na kusema kuwa amekuwa hapigi kilele mitandao kwa sababu hakuumizwa na kutengana kwao. Diamond bila kutaja kuwa anajibu tuhuma alizowahi kutoa Zari kwamba msanii huyo ni kivuruge naye aliamua kuanika wanaume waliowahi kutembea na Zari alipokuwa naye ili ngoma iwe droo. Alisema, wakati wa uhusiano wao alibaini kuwa Zari alikuwa anatoka na mwanamuziki wa Nigeria aitwaye Peter wa Kundi la P-Square na kudai kwamba ushahidi anao.

 

Aidha, alimtaja mwanaume mwingine aliyekuwa akimfanyisha mazoezi Zari kwamba naye alikuwa akitoka na Zari na kusema hata picha zao anazo. Kufuatia matamshi hayo, Zari na wapambe wake waliazisha mashambulizi mapya kwa Diamond ambapo waliposti kila kibaya walichojisikia kumkera nacho mwanamuziki huyo.

 

Zari aliandika hivi kwenye ukurasa wake wa Instagram: “Sasa yale magoti mpaka Sauzi yalikuwa ya nini? Kule kuomba kwako msamaha kwa redio kulikuwa kwa nini? Kwani umekuwa comedian (mchekeshaji) sasa? Usinichafulie maisha bro, yameisha zamani, kubali tu kiki zimekuwa ngumu mjini. Niheshimu tafadhali, nakulelea watoto tena vizuri tu.”

KUHUSU WATOTO

Hivi karibuni moja kati ya magazeti ndugu la hili, Ijumaa Wikienda liliwahi kuandika kuwa, Diamond alikuwa amepigwa stop na Zari kwenda Afrika Kusini wanakoishi wanaye kwa lengo la kuwaona. Jambo hilo alikiri kiana Diamond na kuongeza kuwa mzazi mwenzake huyo amekuwa akiweka figisufigisu kwa msanii huyo kuonana na watoto aliozaa na mwanamke huyo ambao ni Tiffah na Nillan.

 

Katika sakata hili hoja hoti zilizokuwepo mitadaoni zilikuwa ni kumpa madongo Diamond kwamba yanajirudia yaliyomtokea yeye kwa baba yake. “Yeye si amekuwa akisema hakulelewa na baba na yeye watoto wake wanalelewa na wengine, ndiyo ajifunze kuacha kuwafuatisha kina mama wakati mwingine wanafanya mambo mabaya,” aliandika mchangiaji mwingine.

 

DIAMOND APONGEZWA

Pamoja na mambo yote hayo, lakini kitendo cha msanii huyo kumaliza bifu na baba yake watu wengi wamempongeza kwa kusema: “Sasa amekua.” “Mi watu wa kwanza kuwashukuru ni waandishi, wameandika makala na habari nyingi za kumshauri Diamond amalize bifu na baba yake, nadhani ukichanganya na maoni ya wengi kwenye mitandao ya jamii, dogo amesikia, pongezi kwake,”

Comments are closed.