The House of Favourite Newspapers

Baba Diamond: Nikifa Mwanangu Asiguse Jeneza Langu!

Mzee Abdul.

DAR ES SALAAM: Siku chache baada ya msanii wa Bongo Fleva, Mwajuma Abdul ‘Queen Darleen’ kumchana baba yake mzazi ambaye pia ni baba wa msanii wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’, Abdul Juma ‘Baba D’, mzee huyo ameibuka na kusema; “nikifa Queen Darleen asinizike na wala asiguse jeneza langu.”

Kauli hiyo ya mzee Abdul imekuja baada ya Queen Darleen hivi karibuni kufunguka alipokuwa anahojiwa na kituo kimoja kinachorusha matangazo yake kupitia mtandao wa You Tube alipokuwa akimzungumzia mke wa kaka yake, Zarina Hassan ‘Zari The Boss Lady’.

 

MAHOJIANO YENYEWE

Kwenye mahojiano hayo, Queen alimmwagia sifa Zari kwa kusema ana roho nzuri na ndiye mwanamke pekee aliyekuwa anawahimiza angalau yeye na kaka yake (Diamond) wamthamini baba yao.

“Zari ni wifi mzuri, ana roho nzuri na ndiye mtu pekee aliyekuwa anatushauri tumjali baba (mzee Abdul) japo baba mwenyewe kuumwa kwake amekuwa kama mtoto…

“Kwa kweli kwa sasa siwezi kusema baba yangu ni Abdul, baba yangu mimi ni Nasibu…” alisikika Queen mbeleni katika mazungumzo hayo.

Queen Darleen.

WATU SASA

Baada Queen kusema maneno hayo, watu mbalimbali walioiona ‘intaviu’ hiyo walimjia juu na kusema kuwa, kusema baba yake ni kama mtoto ni tusi kubwa na hakustahili kabisa kusema hivyo.

“Hivi anawezaje kumuita baba yake mtoto, halafu eti leo anamkana kuwa si baba yake, laana anayoitafuta ataipata,” alisema mdau mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Mama Caren wa Sinza jijini Dar.

 

BABA DIAMOND AJIBU

Baada ya baba Diamond kusikia mahojiano hayo, alizungumza na Amani nyumbani kwake, Magomeni- Kagera jijini Dar na kueleza hisia zake juu ya mwanaye huyo.

“Yani nimeumia sana. Amezungumza mazito sana kuhusu mimi, sasa niseme tu, na mimi nikifa hata leo asije kabisa kunizika.

“Asisogelee hata jeneza langu, yeye si amesema baba yake siyo mimi, baba yake ni Diamond basi sawa. Hata mimi simtambui. Nikiumwa, nikifanya chochote simhitaji,” alisema baba Diamond huku akibubujikwa na machozi.

Akizidi kumuelezea zaidi Queen, baba Diamond alisema, anasikitika sana binti huyo kutoa maneno mabaya kwake, wakati ni mtoto ambaye alimlea kabla hajawa maarufu.

“Yani kabla hajawa na hilo jina, alikuwa anakuja hapa, anapika na tunakula pamoja leo hii kweli anasema mimi nina akili za kitoto, kwamba nikiumwa nakuwa sina akili? Lini mimi niliumwa nikawa kama mtoto au sina akili?” alihoji baba Diamond na kuongeza:

“Diamond pamoja na ustaa wake wote hajawahi kuniambia maneno mazito kama hayo, hicho kiburi anakitoa wapi mtoto wa kike?”

 

 

Diamond Platinumz.

 

AFUKUNYUA MAMBO

Kama hiyo haitoshi, baba Diamond alisema anashangaa Queen kujiona mjanja sasa hivi wakati yeye ndiye aliyekuwa anampa habari za uchonganishi kipindi cha nyuma akidai mama Diamond ndiyo chanzo cha Diamond kugombana na wapenzi wake akiwemo Wema.

“Yule mtoto mbaya sana. Yeye ndiye alikuwa anakuja hapa anasema ooh… sijui mama Diamond ndiye anayemsababishia Diamond agombane na Wema…ooh… sijui mara hivi kumbe mnafiki mkubwa,” alisema mzee huyo na kuongeza:

“Binafsi hata mimi Zari namkubali maana natambua ana moyo wa huruma na akili kuliko huyu Queen.”

 

HATUA ALIZOCHUKUA

Akizungumzia hatua alizozichukua kuhusu mwanaye huyo, kwanza baba Diamond alisema anamlaani, akifa asimzike lakini pia amechoma moto baadhi ya picha alizokuwa nazo nyumbani kwake.

“Nimezichoma kabisa moto picha zake. Siwezi kuwa na mtoto halafu akanikana hadharani. Acha na mimi nimkane hadharani, hana maana. Asinisaidie kwa chochote, sihitaji msaada wake kwanza,” alisema baba Diamond.

 

TUJIKUMBUSHE

Mzee Abdul aliwazaa Queen Darleen na Diamond kwa mama tofauti, miaka ya nyuma ambapo kama baba, alihakikisha anawapa huduma muhimu ambapo baadaye aliachana na mama yake Diamond, Sanura Kassim ‘Bi Sandra’ na kuanzisha maisha yake.

Wakati Diamond akiwa tayari na jina kubwa, Queen alikuwa angali hana jina kwenye gemu ya Bongo Fleva lakini baadaye, Diamond ‘alimbusti’ kwa kumpa sapoti ya kumuingiza katika kruu lake la Wasafi Classic Baby (WCB) ndipo nyota ya mrembo huyo ilipozidi kung’aa.

Stori: Erick Evarist, Amani

 

BABA DIAMOND: “Nikifa Leo Mwanangu Asiguse Jeneza Langu”

Comments are closed.