Benki ya Dunia Yatoa Magari 11 Mradi wa SWIOFish
BENKI ya Dunia leo imekabidhi magari 11 kwa wakurugenzi na wakuu wa taasisi za Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kupitia mradi wa Southwest Indian Ocean Fisheries Governance and Shared Growth (SWIOFish).
Magari hayo yamekabidhiwa jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Idara Kuu ya Uvuvi Dkt. Yohana Budeba.
Akizungumza katika hafla hiyo kwa niaba ya waziri wa wizara hiyo Dkt. Charles Tizeba, Budeba alisema kuwa lengo la mradi wa Swiofish ni kuboresha usimamizi wa raslimali za uvuvi zilizopewa kipaumbele kikanda, kitaifa na kijamii.
Alisema kuwa anaishukuru Benki ya Dunia kwa imani yao kubwa kwa Tanzania kwa kukubali kufadhili mradi huo kwa kuupatia magari na pikipiki ambazo zilitolewa na kwa halmashauri tano.
Aidha alielezea kwamba mradi wa Swiofish unatekelezwa na baadhi ya taasisi ambazo ni idara kuu ya maendeleo ya uvuvi na idara ya ukuzaji wa viumbe majini, Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (TAFIRI) na sekta binafsi kupitia mpango maalum wa mfuko wa mikopo.
“Ni imani yangu kuwa wanufaika wa magari haya watakuwa waungwana na wazalendo wa taifa hili, katika kutumia na kutunza magari haya kwa umakini na uangalifu mkubwa ili yaweze kutumika kwa muda mrefu.
“Nichukue nafasi hii kuwaomba wakurugenzi na wakuu wa taasisi zitakazopata magari haya kuhakikisha yanatumika kwa malengo na mpango uliokusudiwa,” alisema Budeba.
NA DENIS MTIMA/GPL