Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako pamoja na balozi wa China hapa nchini,WANG Ke leo wameshiriki uwekaji wa jiwe la msingi la sekondari ya mfano ya masomo ya Sayansi mkoani Arusha iliyopewa jina la mkuu wa mkoa huo Mrisho Gambo.
Shule hiyo ya kisasa ambayo kwa mkoa wa Arusha ni ya kwanza itakayokuwa ikiendeshwa kwa mfumo wa kisayansi (STEM) yaani SAYANSI,TEKNOLOJIA, UHANDISI NA HISABATI, Ipo katika kata ya Olasity jijini ambayo hadi sasa tayari madarasa manane ya kisasa yamekamilika na tayari wanafunzi wamenza kuyatumia pia ina maabara nne za kisasa, chumba cha Kompyuta, nyumba za walimu na madawati ambapo madarasa mengine na jengo la utawala bado vikiendelea kujengwa.
Akizungumza baada ya kutembelea na kukagua shule hiyo waziri Ndalichako amepongeza jitihada za uongozi wa mkoa wa Arusha kwa mikakati yake ya kuboresha elimu mkoani humo na nchi nzima ambapo amesema kama serikali wanataka shule hiyo kuwa ya mfano hapa nchini kwa kuwa itakuwa na uwezo wa kuchukuwa wanafunzi wa Sayansi kwa kiasi kikubwa hivyo kusaidia kupata wataalam wakutosha katika Sayansi na technolojia.
“Kwanza nampongeza mkuu wa Mkoa wa Arusha na timu nzima ya uongozi na wananchi kwa kazi nzuri mnayofanya kuboresha elimu katika Mkoa wenu sisi kama wizara tutaendelea kuunga mkono jitihada hizi “alisema Ndalichako
Mkuu wa mkoa wa Arusha mrisho Gambo ametumia fursa hiyo kuwashukuru wadau wote walioshiriki kufanikisha ujenzi wa shule hiyo kwa nanma moja ama nyingine na kusema kuwa kama mkoa wameamua kuwekeza katika elimu kutokana na kutambua umuhimu wa elimu huku akiwatoa hofu wale wote wanaodhani amekuwa akifanya maendeleo hayo kwa nia ya kutaka ubunge wa jiji la Arusha.
Ilikufanikisha ujenzi wa shule hiyo wadau mbalimbali wamechangia katika nyanja mbalimbali ambapo Benk ya I & M imechangia madawati 100 yenye thamani ya shilingi milioni kumi.
Akizungumza katika hafla hiyo Afisa mtendaji Mkuu wa Benki ya I&M Baseer Mohammed amesema Benki hiyo imekuwa ikitoa sehemu ya faida yake kusaidia jamii ambapo imetoa madawati hayo yenye thamani ya shilingi milioni kumi.
“Mhe waziri I & M bank leo imetoa madawati haya 100 kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. John Pombe Magufuli za kutoa elimu bure ili watoto wengi waweze kunufaika na elimu bure” alisema Baseer.