The House of Favourite Newspapers

Benzema Aweka Rekodi Real Madrid Ikiichakaza Liverpool Nyumbani Ligi ya Mabingwa

0

KWA mara nyingine, Liverpool imeangukia pua mbele ya Real Madrid ambapo Vinicius Junior  na Karim Benzema kila mmoja akifunga mabao mawili, huku Victor Osimhen akiipaisha Napoli.

Hii ilikuwa katika mechi za hatua ya 16 bora iliyopigwa juzi Jumanne, Liverpool ikiwa nyumbani ikichapwa mabao 2-5 dhidi ya Real Madrid, Napoli ikishinda kwa mabao 0-2 ugenini dhidi ya Eintracht Frankfurt.

Vinicius alikuwa mchezaji bora wa mchezo huo akifunga mabao mawili na kutoa asisti moja, huku Benzema akiweka rekodi ya kipekee.

Benzema alikuwa ni mchezaji mkubwa zaidi kufunga dhidi ya Liverpool, Anfield katika michuano ya Ulaya akiwa na miaka 35 na siku 46. Pia ameweka rekodi ya kuwa mchezaji aliyefunga katika misimu 18 mfululizo ndani ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, rekodi hiyo inashikiliwa na yeye na Lionel Messi.

Liverpool wameweka rekodi mbovu kwani hawakuwahi kuruhusu mabao zaidi ya manne Anfield katika michuano ya Ulaya.

Kocha wa Real Madrid, Carlo Ancelotti, amesema: “Vinicius Junior ni mchezaji bora na hakuna kama yeye, amefanya kazi kubwa usiku wa leo (juzi), yeye pamoja na Rodrygo walikuwa hatari.

“Naelewa uwepo wa wachezaji wakongwe katika kikosi changu, Kroos (Toni), Benzema na Modric (Luka) wanaongoza kikosi kufanya vizuri, lakini tuna kazi mchezo wa pili, tutapambana.”

Kwa upande wa Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp, alisema: “Vinicius ni mchezaji bora kwa sasa duniani, hilo liko wazi. Lakini bado tuna nafasi ya kushinda mechi yetu ijayo pale Madrid.”

Kwa upande wa Napoli, mambo yalikuwa mazuri kutokana na ubora wa Osimhen aliyefunga bao moja na Kvaratskhelia Khvicha akitoa asisti kwa Giovanni Di Lorenzo.

Napoli ilipata ushindi wa kwanza katika hatua ya mtoano tangu 2011/12 walipoifunga Chelsea mabao 3-1.

Leave A Reply