The House of Favourite Newspapers

Caf yachochea vita ya Aussems, Zahera

Mbelgiji, Patrick Aussems.

KOCHA Mkuu wa Simba Mbelgiji, Patrick Aussems, ameshindwa kujizuia na kuweka wazi kuwa ni lazima wauchukue ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu.

 

Kauli hiyo, ameitoa ikiwa ni siku chache tangu Kocha Mkuu wa Yanga Mkongoman, Mwinyi Zahera kuweka mikakati yao ikiwemo ya kutwaa ubingwa wa ligi na Kombe la Shirikisho Tanzania.

 

Simba iliyofuzu hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika wikiendi iliyopita kwa kuwafunga AS Vita mabao 2-1, hivi sasa ipo katika nafasi ya tatu ya msimamo wa ligi.

Kocha Mkuu wa Yanga Mkongoman, Mwinyi Zahera.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Aussems alisema ni lazima wauchukue ubingwa wa ligi ili washiriki tena kwa mara ya pili mfululizo Ligi ya Mabingwa Afrika. Aussems alisema, hakuna kitakachoshindikana kwao kutokana na ubora wa kikosi chao kinachoongozwa na nyota wengi wenye uwezo wa kuipa ubingwa huo wanaoshikilia.

 

“Tumefanikiwa kufuzu hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika katika hilo tunashukuru, lakini nikiri hayo hayakuwa malengo yetu kwani sisi tulipanga kufika makundi.

 

“Hivyo, basi baada ya kufikia hatua hii tumejifunza vitu vingi hata kama tukitolewa katika hatua hii tuliyofikia kwani ndoto zimetimia kwa asilimia mia moja.

 

“Vitu hivyo, tumepanga kuvifanyia kazi tutakaposhiriki tena kwa mara ya pili mfululizo katika michuano hii kati ya hiyo kupoteza michezo ya ugenini, kitu ambacho sitaki kukiona kikitokea.

 

“Tayari nimeshaweka mipango yangu thabiti ya kuhakikisha tunafanikiwa kuuchukua ubingwa huu wa ligi na kikubwa hatutakiwi kupoteza mchezo wowote wa ligi ili tuwashushe wapinzani wetu Yanga na Azam,” alisema Aussems.

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.