Chama Cha Wahasibu Kuwafuta Wanaokiuka Maadili
Kutoka kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa chama cha wahasibu Tanzania, George Binde, Mwenyekiti, Fred M. Msemwa, Secretary, Dyoya D. James na Mtendaji Mkuu, Valerian Rweyemamu Kaijage.Msemwa (katikati) akitoa ufafanuzi wa jambo.Viongozi hao wakitafakari kujibu maswali yaliyokuwa yakiulizwa na wanahabari ( hawapo pichani).Waandishi wa habari wakifuatilia mkutano huo.
Chama cha Wahasibu Tanzania ‘TAA’ kimesema kuwa kitawafuta katika daftari lake la uanachama wahasibu wanaokiuka maadili ya taaluma au kwenda kinyume na kanuni zinazowaongoza.
Akizungumza na wanahabari leo jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa chama hicho, Dkt. Fred M. Msemwa amesema kwamba chama hicho hakitasita kuwaondoa katika daftari la wanachama mhasibu yeyote atakayekiuka maadili ya taaluma yake kwa kwenda kinyume na miongozo yao ya kazi.
Amesema kuwa anawataka wahasibu na wakaguzi wa hesabu kufanya kazi kwa mujibu wa maadili na taaluma waliyonayo katika umma kwa kufuata miongozo iliyopo katika sheria na 33 ya mwaka 1973 inayosimamia taaluma ya uhasibu na ukaguzi wa hesabu hapa nchini na hivyo kuhakikisha kila uamuzi wa fedha unaofanyika katika taasisi unakidhi matakwa ya kitaaluma kwa matarajio ya wananchi.
Msemwa ameongeza kuwa TAA haitasita kumuondoa mhasibu yoyote atakayebainika na vitendo vya rushwa, wizi, ufisadi na kufanya vitendo vingine kinyume na matarajio ya wananchi.
Hata hivyo chama kitaendelea kuwahudumia wanachama wake kwa kutoa mafunzo ya kitaaluma kwa wanachama wazoefu na wanachama vijana kupitia mpango wa uangalizi wa wanataaluma vijana (Young Accountants Mentoring Programme) wenye lengo la kuongeza weledi kwa wanachama wake.
Hata hivyo chama cha hicho kimeipongeza serikali ya awamu ya tano kwa hatua mbalimbali zilichokuliwa katika kukusanya mapato, hivyo na kuiunga mkono kwa nidhamu ya matumizi na kukusanya mapato ikiwa nguzo kuu ya maendeleo ya nchi kwani bila kukusanya mapato na kutumika ipasavyo taifa haliwezi kufikia malengo.
NA DENIS MTIMA /GPL